WANDERI KAMAU NA VALENTINE OBARA
HATUA ya viongozi wa upinzani kutangaza kuunda vuguvugu jipya jana, imezidisha kiza kuhusu hatima ya Muungano wa Azimio la Umoja-One Kenya.
Wanasiasa hao wakiwa kwenye mkutano wa hadhara katika uwanja wa Kamukunji, eneobunge la Kibra, ulioongozwa na kinara wa ODM, Bw Raila Odinga, walisema wameamua kuunda vuguvugu jipya la Movement for the Defence of Democracy (MDD).
Kulingana nao, wamefanya uamuzi huo ili “kuwahamasisha raia na kuishinikiza serikali kutimiza ahadi ilizotoa kwa wananchi.”
Katibu Mkuu wa ODM, Bw Edwin Sifuna, alisema kuwa vuguvugu hilo litakuwa kama jukwaa lao la kuanza maasi yake makali dhidi ya utawala wa Rais William Ruto kwa “kuwasaliti raia”.
Aliyekuwa waziri wa ulinzi, Bw Eugene Wamalwa, alisema kuelekea mbele, vuguvugu hilo ndilo litakalotumiwa kuvumisha ajenda za upande wa upinzani.
“Tumeanzisha vuguvugu jipya linaloitwa Movement for Defence of Democracy ambalo litakuwa jukwaa la kuishinikiza serikali kutimiza ahadi ilizotoa kwa raia. Ndilo tutakalotumia kuendesha mikutano yetu ijayo katika eneo la Ukambani, Magharibi na kwingineko nchini,” akasema Bw Wamalwa.
Hatua hii imejiri wakati ambapo idadi kubwa ya wanasiasa hasa kutoka Mlima Kenya waliounga mkono azma ya Bw Odinga kwa urais mwaka 2022, wameonekana kuanza kuegemea upande wa serikali ya Rais William Ruto.
Mbunge wa Embakasi Kusini, Bw Babu Owino, amekuwa akidai kuwa pia Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta si mwaminifu kwa Bw Odinga.
Wiki iliyopita, Bw Owino alitoa tena madai hayo akimtaka Bw Kenyatta ahudhurie mikutano yao ya hadhara iwapo kweli bado amejitolea “kusimama na Bw Odinga”.
“Uhuru alikuwa wa kwanza kupewa kazi na Ruto. Ikiwa kweli bado yuko nasi, ajiuzulu hiyo kazi na aje aungane nasi katika mikutano yetu ya hadhara,” akasema Bw Owino, akirejelea kazi ya upatanisho hasa baina ya waasi na serikali ya Demokrasia ya Kongo, ambayo Bw Kenyatta anaongoza.
Akizindua kikundi cha vijana ambao wamejumuishwa katika vuguvugu hilo, Bw Odinga aliashiria kuwa litapanuliwa kitaifa.
“Nyinyi nyote mtaingia katika hili jeshi,” akasema.
Katika miaka iliyopita, Bw Odinga aligeuza baadhi ya mavuguvugu aliyoanzisha kupinga serikali zilizokuwepo, kuwa vyama au miungano ya kisiasa aliyotumia hadi katika chaguzi kuu.
Miongoni mwa vyama na miungano ambayo Bw Odinga alitumia katika miaka iliyopita ni vyama vya LDP na NDP, na miungano ya NARC, CORD na NASA.
Kati ya mavuguvugu hayo yote, chama cha ODM ambacho kiliundwa wakati wa kupinga marekebisho ya kwanza ya Katiba mwaka wa 2005 ndicho kimedumu muda mrefu zaidi.
Uamuzi wa waziri huyo mkuu wa zamani kutoa tangazo kuhusu vuguvugu lake hilo jipya jana, pia huenda ukafasiriwa kuwa kama mwanzo wa muungano mpya.
Hii ni ikizingatiwa kuwa Bw Odinga huchukulia uwanja huo kama wa kihistoria kwa siasa zake.
“Uwanja huu wa Kamukunji ndipo kitovu chetu cha siasa kilizikwa. Ndio maana tuliamua kabla hatujaenda popote kwingine katika taifa la Kenya mpaka tufike Kamukunji kwanza,” akasema.
Baadhi ya masuala ambayo vuguvugu hilo linatarajiwa kupigania ni marekebisho ya sheria za kusimamia Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kabla Uchaguzi Mkuu wa 2027, uhuru wa vitengo vikuu vya kiserikali kama vile mahakama na bunge, ongezeko la gharama ya maisha hasa kutokana na ada za juu za mahitaji muhimu zinazotozwa na serikali.
Wakati huo huo, Bw Odinga alimkashifu Rais Ruto kuhusu suala tata la ulipaji ushuru, ambapo familia ya Bw Kenyatta imedai kuwindwa.
Bw Odinga alisema, wakwepaji ushuru wamejaa katika serikali ya Kenya Kwanza na hivyo basi serikali isipumbaze wananchi kwamba inawasaka kwingine.
Subscribe our newsletter to stay updated