NA KENYA NEWS AGENCY
WANAWAKE na baadhi ya viongozi wa kidini kutoka Kaunti ya Kirinyaga wamepongeza hatua ya kiongozi wa Narc Kenya Martha Karua, kujiunga na Azimio la Umoja.
Mwenyekiti wa chama cha Maendeleo ya Wanawake, tawi la Kaunti ya Kirinyaga, Bi Diana Gicaiyia, jana alisema kwa kujiunga na muungano huo, unaopigiwa upatu kushinda katika uchaguzi mkuu wa Agosti 9, Bi Karua “anajiweka mahala pema katika historia ya taifa hili.”
“Ingawa Bi Karua alikawia kabla ya kufikia uamuzi huo, hatua yake inaonyesha wazi kwamba ameweka maslahi ya taifa hili badala maslahi yake,” Bi Gicaiyia akasema.
Akiongea na wanahabari karibu na uwanja wa kimataifa wa Wanguru mwishoni mwa juma lililopita,
mwenyekiti huyo wa MYW, alisema Bi Karua alionyesha dalili za kujiunga na Azimio la Umoja alipohudhuria mkutano wa chama hicho katika Chuo Kikuu cha Mt Kenya, mjini Thika, juzi.
Bi Gicaiyia na wenzake waliungwa na viongozi wa kidini waliompongeza kiongozi huyo wa Narc Kenya kwa kujiunga na Azimio la Umoja.
Viongozi hao wa kidini wakiongozwa na Askofu Mkuu Boniface Karechio na Pasta Samuel Karuri, walisema ushirikiano wa mgombeaji urais wa muungano huo Raila Odinga na Bi Karua utaleta ushindi mkubwa katika uchaguzi mkuu ujao.