NA SHABAN MAKOKHA
WANDANI wa Rais William Ruto wameapa kuunga mkono pendekezo la kuundwa kwa afisi ya kiongozi rasmi wa upinzani huku kiongozi wa chama cha Roots George Wajackoyah akisisitiza kuwa pendekezo hilo sharti liidhinishwe katika kura ya maamuzi.
Wakiongozwa na Mbunge wa Kiharu Ndindi Nyoro, aliyekuwa Mbunge wa Mumias Mashariki Benjamin Washiali na msaidizi wa rais Farouk Kibet walisema mshikilizi wa afisi hiyo atahakiki utendakazi wa serikali.
Waliongeza kuwa afisi hiyo itachangia kuimarika kwa uwajibikaji serikalini, kwa manufaa ya Wakenya wote.
Wiki jana, Rais Ruto alituma memoranda kwa Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula na mwenzake wa Seneti Amason Kingi aliomba kwamba asasi hizo zisaidie katika kufanikisha marekebisho ya Katiba ili kutoa nafasi ya kuundwa na wadhifa huo.
Huku wakionekana kurejelea kauli ya Rais Ruto ya awali kuwa utawala wake utatoa nafasi kwa upinzani kunawiri, wandani wake wameapa kuunga mkono mswada wa marekebisho ya katiba kufanikisha kuundwa kwa afisi ya Kiongozi Rasmi wa Upinzani.
Bw Washiali alisema afisi hiyo itasuluhisha upungufu uliopo katika Katiba ya sasa ambapo mgombeaji urais anayepata nambari mbili katika uchaguzi wa urais hana nafasi yoyote katika uongozi wa nchi.
Aliwataka Wakenya kukoma kuchukulia kuundwa kwa afisi hiyo kama suala la Raila Odinga au kama ambalo litafaidi Rais Ruto, lakini kwa afisi hiyo italeta faida ya muda mrefu.
“Afisi hiyo haitakuwa yenye manufaa kwa Rais Ruto lakini kwa Wakenya wote kwa sababu itaweka mwongozo wa kisheria ya kuhakiki serikali,” akasema Bw Washiali.
Kiongozi wa upinzani nchini Kenya, Raila Odinga, hana nafasi ya kisheria kuchangia katika utawala bora nchini licha ya kupata jumla ya kura 6.9 milioni katika uchaguzi mkuu wa Agosti 9.
Katika hali ya sasa, wajibu wa kiongozi wa upinzani unatekelezwa na Kiongozi wa Wachache katika Bunge la Kitaifa na Seneti.
Hali kama hii imemwacha mgombea urais aliyeshikilia nambari mbili katika uchaguzi mkuu kutoa matamshi barabarani.
Nyakati zingine kiongozi huyo amekuwa akiitisha mikutano ya hadhara na hata maandamano ya barabarani kupinga maamuzi na mipango ya serikali asiyokubaliana nayo.
Bw Nyoro alisema kubuniwa kwa afisi hiyo kumechelewa.
“Tulihitaji kuwa na afisi hiyo mapema ili tuwe na serikali inayowahudumia watu wake kwa haki na manufaa yao. Kuunda kwa afisi hyo kutaongeza hadhi na majukumu kwa mshikilizi wake,” akasema.
Kulingana na Bw Nyoro ambaye pia ni mwenyekiti wa Kamati ya Bunge kuhusu Bajeti, kiongozi wa upinzani anapasa kupewa nafasi kuhakikisha utendakazi wa serikali moja kwa moja badala ya kutegemea afisi ya kiongozi wa wachache.
“Nyakati zingine kiongozi wa wachache huwa hachukuliwa kama mwenye hadhi ya juu kwa sababu yeye pia ni Mbunge,” akasema Bw Nyoro.
Subscribe our newsletter to stay updated