NA BENSON MATHEKA
INGAWA Naibu Rais William Ruto alidai Jumapili kwamba mchakato wa kuamua mgombea mwenza wake ulichukua saa 17 kuanzia Jumamosi, duru za kuaminika zinasema tayari alikuwa ameamua wadhifa huo ulikuwa wa Bw Rigathi Gachagua.
Ilibainikia kuwa kufikia Jumamosi usiku, washirika wengi wa Dkt Ruto eneo la Mlima Kenya walikuwa wakimuunga mkono Seneta wa Tharaka Nithi, Prof Kithure Kindiki dhidi ya Bw Gachagua, lakini naibu rais akashikilia msimamo wake kuwa mwaniaji wake mwenza ni Bw Gachagua.
Duru zilieleza kuwa Dkt Ruto alizingatia zaidi uaminifu wa mbunge huyo wa Mathira, Kaunti ya Nyeri kwake kwa muda mrefu hata baada ya uhusiano kati yake na Rais Uhuru Kenyatta kusambaratika.
Bw Gachagua amekuwa mtetezi mkubwa wa Dkt Ruto na amekuwa akimkosoa vikali Rais Kenyatta kwa kile amekuwa akidai ni usaliti dhidi ya mtu aliyemsaidia kushinda urais 2013 na 2017.
Katika kikao cha Jumapili cha kutangaza uteuzi huo, Prof Kindiki hakuwepo, ishara kuwa hakuunga mkono uamuzi huo licha ya Dkt Ruto kudai kulikuwa na mashauriano ya kina na maelewano.
Inahofiwa kuwa huenda baadhi ya waliotarajiwa mwaniaji mwenza atoke Mashariki mwa Mlima Kenya wakamkimbia Dkt Ruto.