• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 12:30 PM
‘One Kenya Alliance haitegemei kumuondoa Raila kwa hesabu ya BBI’

‘One Kenya Alliance haitegemei kumuondoa Raila kwa hesabu ya BBI’

Na SAMMY WAWERU

MUUNGANO mpya wa One Kenya Alliance haulengi kumuondoa yeyote katika mahesabu ya Ripoti ya Mpango wa Maridhiano (BBI), amesema kiongozi wa Wiper, Bw Kalonzo Musyoka.

Bw Kalonzo alisema muungano huo unaomjumuisha pamoja na kiongozi wa ANC, Musalia Mudavadi, Moses Wetangula (Ford-Kenya) na Gedion Moi (Moi) hauna nia ya kumuondoa kiongozi wa ODM, Bw Raila Odinga katika mchakato wa BBI kama inavyodaiwa.

“Hakuna jaribio la kumuondoa yeyote katika mchakato wa BBI,” Kalonzo akasema.

“Tunaihitaji ODM na kiongozi wake, Bw Raila Odinga katika muungano wa One Kenya Alliance na unaolenga kuleta Wakenya pamoja na kuwaunganisha. Hatuna njama yoyote fiche,” akaelezea.

One Kenya Alliance ilizinduliwa siku kadha zilizopita, na baadhi ya wandani wa Bw Odinga, akiwemo mbunge wa Suna Mashariki, Junet Mohamed wamedai muungano huo una mkono wa serikali kumuondoa kiongozi wa ODM katika mahesabu ya BBI.

“Nitamtafuta huyo Junet aniambie shida iko wapi,” akasema Bw Kalonzo.

Huku Kenya ikijiandaa kufanya uchaguzi mkuu 2022, Kalonzo alisema miungano kadhaa ya kisiasa itabuniwa.

BBI ilizinduliwa na Rais Uhuru Kenyatta na Bw Raila Odinga, baada ya kufanya salamu za maridhiano, maarufu kama Handisheki.

You can share this post!

Nilikataa chanjo ya masonko nikachanjwa ile ya...

Mafisadi katika utoaji wa chanjo waonywa