NA KAMAU MAICHUHIE
MGOMBEA huru wa urais Nazlin Umar (pichani) amemchagua mwanafunzi wa umri wa miaka 26, kuwa mgombea mwenza wake katika Uchaguzi Mkuu ujao.
Akizungumza katika mahojiano katika jumba la Nation, alieleza kuwa amemchagua Samuel Gichane Mbiu kuwa naibu wake.
Bw Mbiu ni mwanafunzi wa Sheria ya Kimataifa na Haki za Kibinadamu, katika Chuo Kikuu cha Mount Kenya (MKU).
Bi Umar ambaye atakuwa akijaribu bahati yake kwa mara ya nne, ameeleza kuwa yuko tayari.
Aliwania urais manmo 2007 ila akazuiliwa na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka 2013 na 2017 kwa kukosa cheti cha ‘Good Conduct’.
“Nimekubaliwa na IEBC kuwania na niko tayari kuwaletea Wakenya mabadiliko. Nilipata maombi mengi ya Wakenya waliotaka kuwa naibu wangu. Kamati yangu iliwachagua saba na nikamteua Mbiu,” alisema Bi Umar.
Bw Mbiu alikubali jukumu alilopewa na Bi Umar na kueleza kuwa atafanya kazi naye kwa kuwa maono yao kwa taifa la Kenya yanaendana.