• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 11:34 AM
ODM yadai viongozi 4 wamedandia handisheki kujifaidi

ODM yadai viongozi 4 wamedandia handisheki kujifaidi

Na BENSON MATHEKA

CHAMA cha ODM kinalaumu viongozi wa vyama vinne vya kisiasa wanaounga mageuzi ya katiba kwa kudandia handisheki ya kiongozi wa chama chao Raila Odinga na Rais Uhuru Kenyatta kwa lengo la kujifaidi.

Katibu Mkuu wa chama hicho, Bw Edwin Sifuna, amesema kwamba baadhi ya viongozi wa vyama vya kisiasa wamekuwa wakitembelea Ikulu kujadili mswada wa marekebisho ya katiba wa BBI ambao ni matunda ya handisheki kati ya Rais Kenyatta na Bw Odinga.

Bila kutaja majina, Bw Sifuna alisema kuwa ni wanasiasa hao ambao wanapendelewa na baadhi ya maafisa wakuu serikalini ili kumrithi Rais Uhuru Kenyatta na kumzuia Bw Odinga kuingia ikulu.

Ingawa alisema viongozi hao walifanya vyema kuunga mkono BBI, alidai kwamba hawakuwa sehemu ya handisheki kati ya Rais Kenyatta na Bw Odinga.

“Ukweli wa mambo ni kuwa hawana lolote walilochangia katika matunda ya BBI. Hawana maoni yao. Sasa cha kushangaza ni kwamba wanataka kuonekana eti wao ndio wa kuendesha mpango huo wote, ndio unawakuta Ikulu wakinywa chai na mandazi pale wakiambia watu kwamba wao ndio wenye BBI. BBI gani? Wanajua nini kuhusu BBI?” alihoji Bw Sifuna.

Akizungumza katika redio Citizen Alhamisi asubuhi, Bw Sifuna alisema kwamba katika mswada huo, wanasiasa hao hawakuchangia lolote.

“Nini wanaweza kusema ni maoni yao ambayo walitoa? Tunawaambia watulie waache watu wenye maono. Waachie na kuheshimu wale waliowakaribisha kutembea nao katika safari hii,” Bw Sifuna alisema.

Baada ya mswada wa BBI kupitishwa na mabunge 43 ya kaunti, Rais Kenyatta alimwalika Bw Odinga na viongozi wa vyama sita vya kisiasa wanaounga mchakato huo katika Ikulu ya Nairobi kupanga mikakati ya kufanikisha kura ya maamuzi.

Waliohudhuria kikao hicho ni Bw Musalia Mudavadi wa Amani National Congress (ANC), Bw Kalonzo Musyoka wa Wiper, Bw Gideon Moi wa Kanu, Bi Charity Ngilu wa Narc na Bw Moses Wetangula wa Ford Kenya.

Katika taarifa iliyosomwa na Bw Moi, viongozi hao walipongeza mabunge ya kaunti kwa kupitisha mswada huo na kuahidi kukutana Machi 9 na viongozi wengine kupanga mikakati ya kufanikisha kura ya maamuzi.

Chama cha ODM hakikufurahishwa na hatua ya Rais Uhuru Kenyatta ya kuwaalika viongozi wa vyama hivyo kikidai baadhi yao wamekuwa wakimkosoa Bw Odinga.

Washirika wa Bw Odinga hawakufurahishwa na kuungana na ANC, Kanu, Wiper na Ford Kenya katika chaguzi ndogo za maeneobunge ya Matungu Kaunti ya Kakamega, Kabuchai kaunti ya Bungoma na useneta kaunti ya Machakos.

Mabw Mudavadi, Musyoka, Moi na Wetangula wameashiria kwamba wataungana kushindana na Bw Odinga na Naibu Rais William Ruto kwenye uchaguzi mkuu ujao.

ODM kinadai kwamba baadhi ya maafisa wakuu wa serikali wanawaunga wanne hao katika juhudi za kumzuia Bw Odinga kuingia ikulu baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka ujao.

Jana, Bw Sifuna alidai kwamba maafisa hao walimsaidia mgombeaji wa chama cha ANC, Bw Peter Nabulindo kumshinda Bw David Were wa ODM kwenye uchaguzi mkuu wa Matungu ili kumkweza Bw Mudavadi.

You can share this post!

Bintiye Keroche alikiri Lali alimpagawisha kwa mapenzi,...

Aliyefutwa sababu ya ujauzito atuzwa Sh1.4m