• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 1:15 PM
Waandishi wa Thika wapewa hamasisho kuhusu wajibu wao

Waandishi wa Thika wapewa hamasisho kuhusu wajibu wao

Na LAWRENCE ONGARO

WAANDISHI wa habari wamehimizwa kuwa makini wanapoandika habari zao ili ziweze kuaminika.

Walishauriwa kuwa mstari wa mbele kufika kwenye tukio la habari wanazoripoti ili kupata ukweli wa habari hizo.

Baraza la Vyombo vya Habari Nchini Kenya (MCK), liliendesha warsha ya siku moja katika mkahawa mmoja mjini Thika ambako waandishi wa Thika wapatao 20 walihudhuria.

Afisa msimamizi kwa maswala ya mawasiliano MCK Bw Victor Bwire, alieleza kuwa mwandishi anastahili kuripoti jambo aliloshuhudia wala sio la kusikia kutoka kwa watu.

” Ili uweze kujivunia kazi yako kikamilifu kama mwandishi utalazimika kwanza kuchunga usalama wako. Hufai kufanya kazi katika mazingira yanayohatarisha maisha yako,” alisema Bw Bwire.

Aliwahimiza waandishi wawe na umoja wanapofanya kazi yao.

“Kufanya uandishi ukiwa peke yako ni hatari kwa usalama wako. Kwa hivyo, ni vyema kuwa kituo kimoja na wenzako,” alifafanua.

Aliyasema hayo mnamo Ijumaa alipokuwa akiwahamasisha waandishi jinsi ya kujiandaa wanapotekeleza kazi hiyo.

Aliwataka waandishi watakaopata nafasi ya kuripoti uchaguzi mdogo wa Juja utakaofanyika Mei wawe makini kwa kuangazia kila mwaniaji kiti hicho bila kubagua.

“Kila mwaniaji ana haki yake kupewa nafasi ya kujieleza na kupewa nafasi katika vyombo vya habari. Wewe kama mwandishi ni sharti uweke ubinafsi kwa uzito mkubwa.

Alisema waandishi wa habari wanategemewa na mashirika mengi ili kuangazia mambo yao.

Alisema waandishi wamelindwa pakubwa na sheria na kwa hivyo ni bora kuandika ripoti iliyo na ukweli.

Bw Jacob Nyongesa afisa wa mawasiliano katika MCK aliwashauri waandishi wawe makini na habari za uwongo zinazoangaziwa kila mara mitandaoni.

“Habari nyingi ambazo zinaangaziwa mitandaoni huwa sio za kweli bali huwa ni za kuchochea hisia za wasomaji kwa manufaa ya mwandishi mwenyewe,” alisema Nyongesa.

Alisema iwapo mwanahabari ataangazia stori za aina hiyo bila kudhibitisha ukweli wake mhusika huweza kupigwa faini nzito ama kifungo cha jela.

Alisema waandishi wengi huandika habari za uwongo ili kujinufaisha kifedha na kuleta hofu kwa wasomaji.

You can share this post!

Madereva tayari kupaisha mashine zao kuwania alama kwenye...

Baadhi ya watumiaji mitandao ya kijamii wakerwa na agizo la...