• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 6:50 AM
KCSE: Magoha aamrisha polisi wapokonywe simu wasifanikishe udanganyifu wa mitihani

KCSE: Magoha aamrisha polisi wapokonywe simu wasifanikishe udanganyifu wa mitihani

NA MWANGI MUIRURI

WAZIRI wa Elimu Prof George Magoha Jumatatu ametoa amri kuwa maafisa wa polisi wanaolinda harakati za mtihani wa KCSE unaoendelea kote nchini wawe wakipokonywa simu zao za mkononi ili wasishirikishe visa vya udanganyifu.

Prof Magoha akiongea katika Makao makuu ya Kaunti ndogo ya Murang’a Kusini alikofika kunyapara usambazaji wa nakala za mtihani huo alisema kuwa maafisa wa polisi wanaoshiriki zoezi hilo wako na uwezo mkuu wa kuhatarisha uadilifu wa mitihani nchini.

Aidha, waziri huyo alipiga marufuku usafirishaji wa mitihani kwa kutumia magari ya kibinafsi akiteta kuwa “kunao walimu wengine ambao wanatumia huduma hata za matatu kuusafirisha hadi mashuleni mwao.”

Alisema kuwa hali kama hiyo inafanya harakati za kulinda uadilifu wa mitihani ziwe ngumu akiongeza kuwa “ninaamrisha magari rasmi ya shule yawe tu ndiyo yatatumika katika usafirishaji huo.”

Aliteta kuwa matatu ikitoka steji moja hadi nyingine ikipitia kwa kila aina ya chochoro huwezi ukawa na uhakika kwamba visa vya udanganyifu havitekelezwi “na baadhi ya wakora tulio nao katika zoezi hili.”

Alisema kuwa maafisa wa polisi wako na uwezo wa kupiga picha nakala za mtihani na kisha kuzituma kwa mitandao ya udanganyifu na kisha kufikia wanafunzi katika shule zingine kwa kuwa hawaanzii kufanya mitihani hiyo kwa wakati mmoja.

Baadhi ya njama ambazo walio katika mtandao huo wa wizi wa mitihani hutekeleza ni kuchelewesha usambazaji wa nakala hadi baadhi ya mashule ndio kwenye zilifunguliwa ziwe zimepigwa picha na kisha kutumwa kwao.

Hapo ndipo nakala hizo zikishapokelewa hujibiwa harakaharaka na walimu au wengine ndani ya njama hiyo na kupewa wanafunzi ili shule zao zing’are katika matokeo au watoto wao wapate alama za juu.

Prof Magoha alisema kuwa serikali iko macho hasa katika kanda za Magharibi na Nyanza ambako alisema kumezuka habari za ujasusi kuwa njama ya kuiba mtihani huo zinashirikishwa na baadhi ya walimu.

“Tuko na Mwalimu mkuu katika shule moja ya ukanda wa Magharibi ambaye ameshukiwa kuwa na njama ya kupenyeza nakala za kusaidia wizi wa mtihani…Ameamrisha walimu wote waondoke kutoka shule hiyo ndio abakie na mazingara mwafaka ya kuendeleza njama hiyo. Anafaa aaibike sana na nimpe onyo hapa kuwa hataweza kushirikisha ukora huo,” akasema.

Alisema kuna walimu wengine watatu katika Kaunti ya Migori ambao “sijui kama ni wazimu wako nao au ni nini kinawasukuma” kwa kuwa “nao wamefuatiliwa na kutambuliwa kuwa wako na njama hiyo ya kusaidia udanganyifu.”

Prof Magoha aliapa kuwa wote walio katika ajira ya serikali watakaonaswa wakishirikisha wizi wa mtihani huo watafutwa kazi na washtakiwe sambamba na wengine wote ambao watathubutu kushiriki njama hizo.

Mkurugenzi wa Elimu ukanda wa Kati Bi Margaret Lesuda alitoa tahadhari kuwa maradhi ya Covid-19 yashafika katika shule nyingi hapa nchini kwa makali ya ukatili “na ambapo wikendi tu hii imepita tulipoteza walimu wawili wakuu katika shule za msingi huku kwa ujumla tukiwa tumepoteza zaidi ya walimu 15 hadi sasa.”

Alisema kuwa ni suala la dharura kwamba watahiniwa pamoja na wanaoshirikisha zoezi hilo wazingatie masharti ya kiafya hasa katika uvaaji wa maski, kuweka umbali unaopendekezwa na wizara ya afya kutoka mtahiniwa mmoja hadi mwingine, kunawa mikono kwa kutumia sabuni na maji au sanitaiza na pia kuwajibikia dalili za kuugua kwa uadilifu na dharura.

Alisema kuwa “mtihani ambao unaweza ukahatarisha maisha ya watoto au ya wanafunzi na wadau wengine ni hatari hivyo basi kila aina ya tahadhari itekelezwe.”

You can share this post!

Naibu Waziri aishangaa sekta ya matatu kunyima vijana...

Maamuzi tofauti ya korti yaibua utata kesi ya polisi