• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 9:35 PM
Naibu Waziri aishangaa sekta ya matatu kunyima vijana nafasi za kazi

Naibu Waziri aishangaa sekta ya matatu kunyima vijana nafasi za kazi

Na MWANGI MUIRURI

Naibu Waziri wa Spoti, Utamaduni na Turathi za Kitaifa Bw Zack Kinuthia ameteta kuwa sekta ya magari ya uchukuzi wa umma kwa sasa inawanyima vijana wa taifa hili Sh12.8 bilioni kwa mwaka kupitia kupiga marufuklu kazi ya utingo.

Akiongea Jumatano katika Kaunti ndogo ya Kigumo, alisema kuwa udadisi wa hali hiyo ni kwamba baadhi ya wamiliki wa magari hayo licha ya kusukumwa kufanya hivyo na athari za ugonjwa wa Covid-19 “kunao pia wengine miongoni mwao ambao wamefanya hivyo kimakusudi ili kiupounguza gharama za kazi na hivyo basi wajizidishie faida.”

Bw Kinuthia alisema kuwa kuna takriban magari 70, 000 ambayo ni kati ya yote 200, 000 ambayo katika uhudumu wayo, hayana huduma za kondakta na badala yake huwaelekeza abiria wakate tiketi za nauli kabla ya kuanza safari na katika steji barabani, dereva ndiye huwajibikia pia kazi ya Kondakta ya kusukisha na kubeba wengine.

“Ukizingatia mshahara wa chini kabisa wa kondakta ni Sh500 kwa kila mmoja wao kila siku, ina maana kuwa kwa siku wale vijana 70, 000 wangekuwa wameajiriwa kazi hiyo wangekuwa wanajipa Sh35 milioni ambazo kwa mwaka ni Sh12.8 Bilioni,” akasema.

Alisema kuwa hali hii inaangazia ule upungufu wa ushirika kati ya serikali na sekta ya kibinafsi katika kuunda nafasi za kazi.

“Ikiwa sekta hii ambayo kwa asilimia 80 iko mikononi mwa vijana inaweza ikawanyima wenzao 70, 000 nafasi za kujipa riziki, ina maana kuwa kuna shida kuu ambayo inafaa ijadiliwe na itafutiwe suluhu,” akasema.

Bw Kinuthia alisema kuwa wakati serikali inajizatiti kupambana na umasikini kupitia kutoa mazingara mwafaka ya kuunda ajira na mapato, kunafaa kuwe na mashauriano kati ya sekta hii ya uchukuzi pamoja na serikali ili kubaini hasa kinachozima nafasi hizo za kazi kupokezwa vijana.

Mwenyekiti wa Muungano wa Wamilki magari ya uchukuzi Mlima Kenya Bw Micah Kariuki alisema kuwa tangu sekta hii ya matatu iiwekwe chini ya uratibu wa vyama vya ushirika au makampuni, kanuni za utendakazi zilianza kuwekwa kwa mtazamo wa kibiashara.

“Maamuzi mengi kwa sasa huzingatia jinsi ya kuendesha biashara ili iunde faida kupitia kuvutia wateja wengi iwezekanavyo. Kazi ya utingo kwa wakati mwingine imekuwa changamoto kuu kufuatia tabia za matamshi na matendo kwa wateja ambapo husemwa na wengi hukera,” akasema.

Bw Kariuki aidha alisema kuwa tangu kuzuke ugonjwa wa Covid-19 na masharti yakawekwa kuwa magari ya uchukuzi wa umma yapunguze idadi ya abiria hadi asilimia 60 ya uwezo wa upakiaji, kiti cha kondakta kilionekana na wengi wa mameneja wa uchukuzi kuwa kinaweza kikaondolewa ili kiletee mwenye gari pesa.

Ni magari tu yale ambayo hayabebi kutoka steji maalum na kusafirisha wateja wake moja kwa moja almaaurufu “Express” ambayo yamekuwa yakiajiri makondakta kwa kuwa wanahitajika katika harakati za kuwasaka abiria kutoka steji moja hadi nyingine katika barabara ya uhudumu.

Bw Kariuki alisema kuwa ikiwa makali ya ugonjwa wa Covid-19 yatapunguka, nayo serikali ijizatiti na iteremshe bei ya mafuta, ipige msasa mfumo wake hasi wa ushuru na hatimaye iondoe ufisadi wa maafisa wa trafiki barabarani, basi biashara inaweza ikapanua utenda kazi wa faida na iishie kuunda nafasi hizo za kazi ambazo kwa sasa zimepotea.

You can share this post!

Wazazi walia kanuni za corona zinaumiza watahiniwa wa KCSE

KCSE: Magoha aamrisha polisi wapokonywe simu wasifanikishe...