• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 5:50 AM
CHOCHEO: Chunga ‘mboch’ asijepasha joto kitanda chako

CHOCHEO: Chunga ‘mboch’ asijepasha joto kitanda chako

 

Na BENSON MATHEKA

BAADA ya miaka sita ya ndoa, Eve aligundua kwamba mumewe alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na kijakazi wao.

Alikasirika sana lakini mumewe akamwambia kwamba anafaa kujilaumu mwenyewe. Alimwambia kwamba alimuachia kijakazi wao majukumu ya mke.

Baada ya kutafakari, Eve aligundua kwamba makosa yalikuwa yake. Alikubali kwamba alikuwa amempuuza mumewe huku akimwachia kijakazi wao kazi ya kumpikia na hata kumshughulikia kwa mahitaji yote ya nyumbani.

“Nilibaini kwamba nilikuwa nimefeli katika majukumu yangu kama mke naye akamtwaa aliyekuwa akimshughulikia. Nilijuta kwa kumwachia kijakazi kazi yangu kama mke. Niliamua kurekebisha hali hata baada ya kumfuta kazi mwanadada huyo na nikatia bidii katika kumshughulikia mume wangu,” Eve kafunguka.

Kulingana naye, ni makosa kwa wanawake kuwaamini wafanyakazi wao wa nyumbani hadi kiwango cha kuwaachia majukumu ya kuwatunza waume zao.

“Kufanya hivi ni kutelekeza mumeo na kujiweka katika hatari. Ni rahisi mwanamume kuingiwa na hisia za mapenzi kwa kijakazi anayemshughulikia kwa kila kitu nyumbani. Hii ndiyo inafanya wanawake wengi kupokonywa waume zao na wafanyakazi wa nyumbani,” asema Eve.

Majukumu

Kulingana na Sally Achieng, mshauri wa wanandoa wa shirika la Fountain of Love jijjni Nairobi, wanawake huwa wanasahau kwamba wao ndio wameolewa na sio wafanyakazi wao wa nyumbani.

“Daima kumbuka kuwa wewe ndo umeolewa. Wajibika kikamilifu ikiwa hautaki kupokonywa mumeo na huyo mwanadada unayemwachia jukumu la kwako. Kazi ya kuwa mke haiwakilishwi kamwe,” asema Achieng.

Mshauri huyu anasema wafanyakazi wa nyumbani wanafaa kumsaidia mke katika baadhi ya majukumu yasiyohusu waume zao moja kwa moja.

“Inashangaza baadhi ya wanawake hupatia vijakazi jukumu la kuamsha waume zao na kuwaandalia kiamsha kinywa na hata kuwachagulia suti za kuvaa. Kufanya hivi ni kukabidhi ‘mboch’ majukumu yako na kumpa nafasi ya kukupokonya mume au kuchepuka naye,” asema Achieng.

Ingawa wataalamu wanasema baadhi ya wanaume hutawaliwa na tamaa kiasi cha kufanya mapenzi na wafanyakazi wa nyumbani, wataalamu wanasema wanawake walioolewa wanafaa kutekeleza majukumu yao kikamilifu.

“Kamwe usimpatie au kumwachia mtu yeyote kazi inayoweza kumtia mumeo kwenye majaribu. Wacha watu wengine wafanye mambo mengine lakini zingatia kwamba unafaa kujukumika kwa mumeo peke yako,” asema Ashley Kombo wa shirika la Families For Tomorrow.

Kombo anasema mwanamume huwa anashawishika na kuchotwa akili na mwanamke yeyote anayewajibika kwake na masuala ya nyumbani.

“Kinga ndoa yako kwa kumtenga mjakazi na mumeo. Acha alee watoto chini ya uelekezi wako lakini usimpatie jukumu la kumkaribia mumeo. Kinga mkeo asitumbukie katika majaribu ya kumchangamkia house-boy kwa kumpa haki yake ya ndoa anapohitaji. Hakikisha humuachi kwa muda mrefu na yaya/kitwana nyumbani peke yao,” asema Kombo.

“Mke anayefahamu majukumu yake anajua kumkinga na kumshughulikia mumewe ili asitumbukie katika majaribu ya kuchangamkia wanawake wengine wakiwemo wafanyakazi wa nyumbani. Hii inawezekana kwa kumtengea yaya majukumu yake,” asema.

Achieng anasema kwamba baadhi ya wanawake huchangia uchepukaji kwa kutowekea wafanyakazi wa nyumbani mipaka ya majukumu.

Lakini kulingana na Simon Njagi wa kituo cha Liberty Center, hakuna sababu inayoweza kushawishi mwanamume kushiriki tendo la ndoa na mjakazi isipokuwa tamaa na kumkosea mkewe heshima.

“Huwezi kutakasa makosa ya kuzini na mjakazi kwa kudai mkeo alimwachia majukumu yake. Hauwezi kutakasa tamaa yako ya kulala na yaya kwa kudai mkeo alikutekeleza. Mtu anayemheshimu mkewe hawezi kumsaliti kwa vyovyote,” asema.

Hata hivyo anakiri kwamba wanawake wanafaa kuhakikisha kuna mipaka ya majukumu ya wafanyakazi wa nyumbani na majukumu yao kwa waume zao.

You can share this post!

FUNGUKA: ‘Nacheza mechi za majuu pekee’

TAHARIRI: Tuendee nishani nyingi zaidi Tokyo Olimpiki