• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 8:55 PM
JAMVI: Ruto kupokelewa kishujaa Kisumu kunaashiria nini?

JAMVI: Ruto kupokelewa kishujaa Kisumu kunaashiria nini?

Na CHARLES WASONGA

HISIA mseto imeibuka kuhusu mapokezi mazuri ambayo Naibu Rais William Ruto alipokea mjini Kisumu Jumanne wakati wa sherehe za Siku Kuu ya Madaraka Dei mjini Kisumu.

Wandani wake, haswa wamechangamkia hatua ya wakazi wa eneo la Kondele kumshabikia Dkt Ruto kwa mbwembwe na hoi hoi alipokuwa akiondoka uga mpya wa michezo wa Jomo Kenyatta baada ya kukamilika kwa sherehe hizo zilizoongozwa na Rais Uhuru Kenyatta Jumanne.

Baadhi yao walisema mapokezi hayo yaliashiria kuwa wakazi wa kitongoji hicho na Nyanza kwa ujumla sasa wamezinduka na kuamua kukumbatia sera za vuguvugu la hasla za kutetea masilahi ya wanyonge.

Lakini wafuasi wa ODM wamepuuzilia mbali dhana hiyo wakisema wakazi wa Kondele, na Kisumu kwa ujumla sasa “wamekomaa na wamebadilisha mienendo yao baada ya kuingiwa na injili ya maridhiano iliyoasisiwa na handisheki kati ya Rais Kenyatta na Raila Odinga.”

Kinyume na matajio ya wengi, wakazi hao, haswa vijana, walisimamisha msafara wa Naibu Rais wakimtaka awahutubie licha ya kwamba wao ni wafuasi sugu Bw Odinga ambaye ni kiongozi wa ODM.

Lakini Dkt Ruto, ambaye ni hasimu mkubwa wa kisiasa wa Waziri huyo mkuu wa zamani, alijibu kwa kuwapungia mikono kwa sababu gari lenye mitambo ya sauti lilikuwa mita kadhaa nyuma.

Mtaa wa Kondele, haswa karibu na daraja la juu kwa juu (Flyover), umekuwa kitovu cha machafuko ya kisiasa tangu 2007 ambako wafuasi wa ODM walikabiliana na polisi wakipinga kile walichodai ni Bw Odinga kuibiwa kura za urais.

Kwenye mahojiano na Jamvi, mshiriki mkuu wa chama cha United Democratic Alliance (UDA) eneo la Nyanza, Eliud Owallo, alisema kuwa mapokezi ambayo Dkt Ruto alipata Kisumu yanaashiria kuwa kampeni za kuelekea uchaguzi mkuu ujao zitaongozwa na sera wala sio siasa za vyama au watu binafsi.

“Yale ambayo Wakenya walishuhudia Kisumu na haswa eneo la Kondele juzi, yanaonyesha watu wa Nyanza wamezinduka. Wameona mwanga na ifikapo uchaguzi mkuu ujao, bila shaka watafanya maamuzi yao sio kwa misingi ya maagizo kutoka chama fulani au mwanasiasa fulani, bali sera ambazo zitabadilisha maisha yao,” akasema.

“Hivi karibuni Dkt Ruto atarejea Nyanza kwa ziara ya kukutana na wananchi moja kwa moja na kusikiza matakwa ya mahasla mashinani,” akaongeza Bw Owalo ambaye mnamo 2013 alihudumu kama mkurugenzi mkuu wa sekritariati iliyoshirikisha kampeni za urais za Bw Odinga.

Kwa upande wao wabunge Nelson Koech (Belgut) na Oscar Sudi (Kapseret) walisema kuwa mapokezi ambayo Dkt Ruto alipata Kisumu ni kielelezo cha kiwango ambacho “injili” ya hasla imepenyeza katika ngome hiyo ya kisiasa ya Bw Odinga.

“Sasa wakazi wa Kondole na Kisumu kwa ujumla sio mali ya mtu binafsi. Wameonyesha kuwa hawataki kuachwa nyuma katika wimbi hili la mageuzi. Bila shaka wanataka kuvuna matunda ya sera za kiuchumi zinazoratibiwa na vuguvugu la hasla. Wamechoshwa na ahadi tasa za ODM ambazo hazijawakwamua kutoka lindi la umasikini miaka nenda miaka rudi,” Bw Sudi akaambia Taifa Jumapili.

Kwa upande wake Bw Koech aliweka ujumbe shukrani, kwa lugha ya dholuo, kwenye kaunti yake ya twitter uliosema hivi: “Erokamano Kisumo. Wabiro duogo kendo Kondele” (Asanteni watu wa Kisumu. Tutarejea tena Kondele).

Wandani wengine wa Naibu Rais waliochangamkia mapokezi yake Kisumu ni aliyekuwa Seneta wa Kakamega Bonny Khalwale na Mbunge wa Gatundu Kusini Moses Kuria.

Lakini Mwenyekiti wa ODM John Mbadi alipuuzilia kauli za wakereketwa wa UDA wakazi wa Kisumu wamekumbatia chama hicho akizitaja kama “ndoto za mchana”.

“Jumanne haikuwa siku ya siasa. Ilikuwa ni siku ya kipekee kwa wakazi wa Kisumu na hata Kondele kwani kwa mara ya kwanza katika historia ya taifa hili, wao ndio walikuwa wenyeji wa sherehe muhimu ya kitaifa kama Madaraka Dei. Bila shaka ilikuwa ni siku ya fuhara na nafasi yao ya kukaribisha viongozi wote kwa msisimko, akiwemo Naibu Rais William Ruto,”

“Wale wanaodai msisimko ulioshuhudiwa miongoni mwa wakazi wa Kondele unaonyesha kuwa wamebadili msimamo wao wa kisiasa wanaota mchana. Kisumu na Nyanza, ingali ngome ya ODM na itasalia kuwa hivyo,” akaeleza Bw Mbadi ambaye ni kiongozi wa wachache katika Bunge la Kitaifa.

Lakini mchanganuzi wa siasa za Luo Nyanza Tom Mboya anakinzana kimawazo na mbunge huyo wa Suba Kusini.

Kulingana na mhadhiri huyu wa Chuo Kikuu cha Maseno, yale yaliyoshuhudiwa Kisumu Jumanne yanaashiria kuwa siasa za eneo hilo na Nyanza kwa ujumla yamechukua mkondo mpya.

Kwamba wakazi na viongozi wa kisiasa wameng’amua kuwa hawatapoteza chochote kwa kukumbatia vyama au mirengo tofauti ya kisiasa kando na wake Bw Odinga na chama chake cha ODM.

“Naamini kuwa mapokezi mazuri aliyopewa Naibu Rais kule Kondele, yalipitisha ujumbe fulani wa kisiasa. Aidha, ilikuwa ni onyo kwa Raila Odinga na chama chake cha ODM kwamba endapo hawatapigania mahitaji ya kimsingi ya wakazi hao basi waweza kuunga mkono mirengo pinzani 2022,” anaeleza Dkt Mboya.

Anabashiri kuwa wakazi wa Nyanza huenda wakaendeleza mtindo waliouanza 2013 wa kuwachagua wabunge na hata magavana wasiodhaminiwa na ODM. Kwa mfano, katika uchaguzi mkuu wa 2017, ODM ilipoteza viti vya ubunge vya Kisumu Mjini Mashariki, Kisumu Mjini Magharibi na Uriri vinavyoshikiliwa na Olago Aluoch (Ford Kenya), Shakeel Shabiri (Kujitegemea) na Peter Masara (Kujitegemea), mtawalia.

You can share this post!

Hydroponic: Mfumo bora wa kilimo kukwepa kero ya magonjwa

2022: Kuna dalili Uhuru atasema ‘Raila Tosha’