• Nairobi
  • Last Updated May 5th, 2024 6:07 PM
2022: Kuna dalili Uhuru atasema ‘Raila Tosha’

2022: Kuna dalili Uhuru atasema ‘Raila Tosha’

Na BENSON MATHEKA

DALILI za wazi kuwa Rais Uhuru Kenyatta huenda akamtangaza kiongozi wa chama cha ODM, Raila Odinga kuwa mrithi wake, zilijitokeza baada ya kiongozi wa nchi kuahidi kwamba wataendelea kushirikina kwa manufaa ya Wakenya siku zijazo.

Akizungumza akiwa Kisumu alipoongoza sherehe za 58 za Madaraka Dei, Rais Kenyatta alisema kwamba ataendelea kushirikiana na Bw Odinga ili kuhakikishia Kenya ustawi.

“Ninataka kusema hapa leo kwamba hata iweje siku zijazo, nitaendelea kushirikiana naye na viongozi wote wa Kenya na Wakenya ili kufanya Kenya, Afrika Mashariki na Afrika kuwa bora, iliyoungana zaidi na yenye ustawi,” alisema Rais.

Ingawa wawili hao wamekuwa wakitetea ushirikiano wao kufuatia handisheki yao ya Machi 9 2018, wamekuwa wakisema haihusu uchaguzi mkuu wa 2022, tamko la Jumanne linaashiria kuwa kuna uwezekano Rais Kenyatta atamtangaza Bw Odinga kuwa chaguo la mrithi wake.

Wachanganuzi wa siasa wanasema kwamba kauli yoyote ya kiongozi wa nchi wakati wa sherehe ya kitaifa kama Madaraka haiwezi kupuuzwa.

“Kumekuwa na kila dalili kwamba ushirika wao wa kisiasa unahusu uchaguzi mkuu wa 2022 japo wamekuwa wakikanusha. Kwa kusema ataendelea kushirikiana naye ni kumaanisha kwamba handisheki yao inahusu zaidi ya kubadilisha katiba,” alisema mchanganuzi wa siasa Peter Katana.

Anasema kauli ya rais ililenga kuhakikishia ngome yake ya Nyanza kwamba hatamsaliti baadhi ya viongozi wa ODM wanavyohofia.

Mapema mwaka huu, baadhi ya viongozi wa ODM walidai kwamba washirika wa rais walikuwa wakipanga siasa za urithi kwa kumtenga Bw Odinga.

Hii ilifuatia madai kwamba Rais Kenyatta alikuwa akiunga muungano wa One Kenya Alliance unaoshirikisha mwenyekiti wa chama cha Kanu Gideon Moi, kiongozi wa chama cha Amani National Congress (ANC) Musalia Mudavadi, mwenzake wa Wiper Kalonzo Musyoka na Moses Wetangula wa Ford Kenya.

Hofu ya viongozi wa ODM, ilimfanya Rais Kenyatta kuchukua hatua ya kuhakikishia Bw Odinga kuwa handisheki ingali imara na hana nia ya kumsaliti.

Duru zinasema Rais Kenyatta ameanza mikakati ya kupatanisha vinara wa One Kenya Alliance na Bw Odinga kwa lengo la kuepusha migawanyiko ambayo Naibu Rais William Ruto anaweza kutumia kushinda urais kwenye uchaguzi mkuu wa 2022.

“Kuna mikakati ya kupatanisha vyama vinavyounga BBI na kilele chake kitakuwa kumtangaza Odinga kuwa nahodha wa timu moja kubwa itakayomkabili Dkt Ruto kwenye uchaguzi mkuu wa 2022. Kwa maoni yangu, hivi ndivyo rais aliashiria alipoahakikishia wafuasi wa Bw Odinga eneo la Nyanza kwamba atamuacha,” alisema mbunge mmoja wa Jubilee ambaye aliomba tusitaje jina asionekana kumwaga mtama bila idhini.

Hata hivyo mwenyekiti wa chama cha ODM, John Mbadi alitaja kauli ya rais kuwa sababu kuu ya handisheki.

“Nafikiri kile ambacho rais alisisitiza ni kwamba handisheki yao ilihusu siku zijazo za nchi na sio kwa maslahi ya kibinafsi,” alisema Bw Mbadi.

Akizungumza na kituo kimoja cha redio cha lugha ya Dholuo mnamo Jumatatu, Bw Odinga aliambia wakazi wa ngome yake ya Nyanza kwamba uchaguzi mkuu wa 2022, utakuwa uwindaji mkubwa na kwamba eneo lao halitakosa minofu. Wachanganuzi wa siasa wanasema hii pamoja na kauli ya rais kwamba atatembea naye siku zijazo ni sawa na kuwaandaa wafuasi wa Bw Odinga kwa tangazo la “Raila tosha” kabla ya 2022.

“Hii ilikuwa kuwaandaa wafuasi wa Bw Odinga kwa tangazo kubwa. Kuna uwezekano litakuwa ni baba anatosha. Muhimu kukumbuka ni kuwa Rais Kenyatta amewahi kusema kwamba rais anaweza kutoka nje ya jamii mbili zilizowahi kutoka rais,” alisema mchanganuzi wa siasa Jacob Kituyi.

Kwenye hotuba yake ya Madaraka Dei, Rais Kenyatta alimshehenezea sifa Bw Odinga kwa hatua waliyochukua kutuliza nchi baada ya joto la kisiasa lililopanda baada ya uchaguzi mkuu wa 2017.

Hata hivyo baadhi ya wanasiasa wanahisi kwamba kauli hiyo ilikuwa ya kisiasa kufurahisha wafuasi wa Bw Odinga katika Nyanza tu.

“Mwelekeo kwa siasa za urithi utabainika baada ya Agosti mwaka huu kwa kutegemea hatima ya mswada wa kura ya maamuzi,” asema mdadisi wa siasa, Geff Kamwanah.

You can share this post!

JAMVI: Ruto kupokelewa kishujaa Kisumu kunaashiria nini?

JAMVI: Wazee wa Pwani wanakosa sauti ya kunguruma kisiasa