• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 2:25 PM
Wanafunzi 94 kutoka Thika kupata ufadhili masomoni

Wanafunzi 94 kutoka Thika kupata ufadhili masomoni

Na LAWRENCE ONGARO

WANAFUNZI kutoka familia maskini wapatao 94 katika kaunti ndogo ya Thika watanufaika na mpango wa serikali kuwasaidia kusoma katika shule za upili.

Waziri wa Elimu Prof George Magoha amezuru Thika mnamo Alhamisi na kushuhudia wanafunzi hao wakihojiwa na washika dau katika sekta tofauti.

Kila mwanafunzi na mzazi wake walihojiwa wakati tofauti ili kupata picha kamili ya familia yao, kabla ya kupata nafasi hiyo.

Waziri amewahimiza wadau wote walioshiriki katika uteuzi huo kuhakikisha kila mwanafunzi anatendewa haki bila kubaguliwa kwa njia yoyote ile.

Wanafunzi wapatao 171 walifika kujaribu kupata fursa kwenye uteuzi huo huku wakiwa wameandamana na wazazi wao.

Maswali mengi yaliangazia kuhusu familia, maeneo wanakotoka, uhusiano wa mzazi na mtoto, na kuhusu hali ya maisha kwa ujumla, pamoja na matarajio yao ya siku za usoni.

Kati ya wanafunzi hao wote waliohojiwa, ni 86 watakaonufaika na mpango wa Elimu Scholarship Program halafu wanane nao watapata nafasi ya usaidizi kupitia mpango wa Wings To Fly ambao ni udhamini kutoka benki ya Equity.

Prof Magoha ameeleza kuwa serikali imejitolea kuona ya kwamba wanafunzi wasio na uwezo wa karo wanapata nafasi ya kuendelea na masomo yao bila kutatizwa.

“Nitahakikisha ninatekeleza wajibu wangu katika wizara nikifuata maagizo ya Rais Uhuru Kenyatta. Pia nataka maafisa wakuu katika Wizara ya Elimu waniunge mkono,” alifafanua waziri huyo.

Amezipongeza; benki ya Equity, chini ya mkurugenzi wake James Mwangi, KCB, na benki ya Co-operative kwa kujitolea pia kuona ya kwamba zinatoa ufadhili kwa maswala ya elimu.

Waziri alitoa changamoto kwa wazazi na kuwashauri wasibague shule wanazopeleka wana wao kwa sababu shule zote zinafundisha masomo sawa kuambatana na mtaala uliotolewa na Wizara ya Elimu.

You can share this post!

Kizaazaa kortini baada ya kasisi aliyetisha mpenziwe...

Nina kiu ya kunolewa na kocha Ronald Koeman – Memphis...