• Nairobi
  • Last Updated May 6th, 2024 8:55 PM
Kizaazaa kortini baada ya kasisi aliyetisha mpenziwe kuachiliwa huru

Kizaazaa kortini baada ya kasisi aliyetisha mpenziwe kuachiliwa huru

KITAVI MUTUA

KUZUKA kizaazaa Jumatano katika majengo ya mahakama ya Kitui baada ya kasisi mmoja wa kanisa Katoliki aliyeshtakiwa kwa jaribio la kumuua mpenziwe na mtoto aliyezaa naye, kuachiliwa huru.

Kasisi Japheth Mwove Kimanzi aliachiliwa na Hakimu Mkuu Stephen Mbungi, hatua iliyosabisha waathiriwa kusababisha sokomoko na kupiga mayowe wakidai kunyimwa haki.

Mhasiriwa, Veronica Musali Mutua, aliangua kilio ndani ya majengo ya mahakama punde tu hakimu huyo alipomaliza kusoma uamuzi wake.

Kulingana na Mbungi, hakukuwa na ushahidi wa kumhusisha mshtakiwa na kosa la kushambulia na kumuumiza mama na mwanawe.

Huku akiwa amembeba mwanawe mwenye umri wa miaka tisa mgongoni, Bi Mutua alilia akidai kuwa mahakama imeamua, kimakusudi, kumpendelea kasisi huyo, ambaye ni mpenzi wake wa zamani, aliyegeuka na kumdhulumu.

“Nawaomba watu wenye nia njema kuingia kati suala hili, kwa kukata rufaa dhidi ya uamuzi huu ili mtoto wangu apate haki,” mama huyo akasema huku akidondokwa na machozi.

Mtoto huyo ni kiziwi na kipofu kutokama na madhara aliyopata kwa kushambuliwa na mshtakiwa.

Kasisi Kimanzi aliondoka kortini huku akitabasamu baada ya kuondolewa makosa hayo ambayo adhabu yake ni kifungo cha miaka miaka kumi gerezani.

Hata hivyo, Kasisi huyo amevuliwa wadhifa huo na Kanisa Katoliki kwa kushtakiwa kwa kosa la kushambulia na kumjeruhiwa mpenzi wake na mwanawe. Kesi hiyo imekuwa ikiendelea kwa muda wa miaka sita tangu mwaka wa 2015.

Ndani ya kipindi hicho, ufichuzi ulitolewa kuhusu jinsi Kimanzi alijaribu kuharibu ushahidi uliomhusisha na madai kuwa ndiye baba wa mtoto. Maelezo hayo yalitolewa wazi kortini kama thibitisha kuwa alivunja kanuni ya kanisa Katoliki inayohitaji makasisi wake kutoshiriki uasherati au kuoa.

Nao upande wa mashtaka ulikuwa ukijitahidi kuhakikisha kuwa kasisi huyo wa zamani amepatikana na hatia ya kuwashambulia Bi Mutua na mwanawe na kuwajeruhi.

Kisa hicho kilitendeka mnamo Novemba 16, 2015. Mtoto huyo kwa jina Lilian Mwikali alilemaa kwa kupoteza uwezo wa kuona na kusikia. Vile vile, alijeruhiwa kwenye miguu.

Licha ya ripoti ya uchunguzi wa chembechembe za DNA kuwasilishwa mahakamani, Kimanzi ambaye zamani alisimamia Parokia ya Kabati katika Dayosisi ya Kanisa Katoliki Kitui, alidinda kuungama kwamba ndiye babake mtoto huyo.

Vile vile, alikataa kuwajibikia malezi ya mtoto huyo na kuhujumu juhudi zote za familia ya msichana huyo za kutaka apate haki.

Mahakama iliambiwa kuwa Bi Mutua, wakati huo akiwa mwanafunzi wa kidato cha kwanza, alivutiwa na Bw Kimanzi kwa biskuti, pesa na vito vya kujirembesha. Wakati huo, Novemba 2015, mwanamume huyo alikuwa akihudumu kama kasisi katika Parokia ya Nuu.

BI Mutua aliambia mahakama kwamba kasisi huyo alimshawishi washiriki mapenzi alipokuwa mwanafunzi katika Shule ya Upili ya Mwambiu, mjini Mwingi. Hata hivyo, baadaye alimgeuka na kumtisha, kumdhulumu n ahata kumhonga ili asitoboe siri kuhusu uhusiano wao.

“Niliacha shule kwa aibu na kuwavunja moyo wazazi wangu. Wenzangu walinichekelea kwa kufanya urafiki na kasisi. Hata hivyo, kumlea mwanangu kwa miaka hiyo yote,” akasema kwenye ushahidi wake kortini.

Tafsiri: CHARLES WASONGA

  • Tags

You can share this post!

Italia wakung’uta Uswisi na kuingia hatua ya 16-bora...

Wanafunzi 94 kutoka Thika kupata ufadhili masomoni