• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 5:50 AM
DONDOO: Jombi achanganywa na demu mgeni plotini aliyemwomba mwiko

DONDOO: Jombi achanganywa na demu mgeni plotini aliyemwomba mwiko

NA NICHOLAS CHERUIYOT

KAPERA mmoja alipandwa na mzuka kipusa aliyehamia ploti anakoishi juzi, alipomuomba mwiko asonge sembe.

Duru zasema jamaa alikuwa kwake akitulia kidosho huyo, mwenye umbo la kuvutia, alipobisha mlangoni kisha akamuomba amsaidie na mwiko wake aandae ugali.

Kipusa alisema haya tabasamu likiwa usoni pake.

Jamaa alimpa kipusa mwiko huo kisha akatoka nje kuuliza marafiki iwapo kidosho alitaka mwiko tu ama alikuwa na nia nyingine.

“ Baadhi yao walimwambia ni kiu yake ya muda mrefu iliyomsukuma awaze zaidi ya mwiko wa kawaida huku wengine wakimwambia hiyo ni ishara demu huyo anammezea mate,” mdaku akasema.

***

Msupa atimua Kalameni dume suruali kwa kutojua kupenda

Na JANET KAVUNGA

JOMBI aliyekuwa akijigamba kwa kukwachua demu sonko mtaani hapa alijua hajui baada ya mwanadada huyo kumtimua kwake akimlaumu kwa kutotosha mboga.

Jamaa alikuwa ameishi na demu huyo kwa miezi saba mambo yalipomwendea kombo. Mwanadada alidai kwamba hakupata alichotarajia kutoka kwa jamaa.

“Kazi yako ni kujigamba mtaani kwamba umepata demu wa nguvu ilhali hujui mapenzi. Nilidhani utanipa raha kama dume kamili lakini kazi yako ni domo na kulewa kisha unakoroma usiku kucha,” demu alimweleza jamaa na kumtaka afunge virago na kuona paa la nyumba yake.

Inasemekana baada ya kumtema jamaa, demu alimchangamkia mmoja wa wale ambao jombi alikuwa akiwaringia.

***

Pasta akataa polo aliyehama kanisa kuposa binti yake

JOHN MUSYOKI

MPANGO wa Kalameni wa hapa kutaka kumuoa binti ya pasta uligonga mwamba mchungaji huyo alipokataa posa akidai jamaa aligura kanisa lake kwa dharau.

Polo alipanga kumposa demu na akatembelea kwao nyumbani akiandamana na jamaa na marafiki zake . Walifika kwa demu kwa magari ya kifahari na bashasha za kila aina.

Jamaa alipoeleza mipango yake ya kumposa demu na kumuoa, baba ya kipusa alimtazama kwa macho makali na kuwaka kwa hasira.

“Hapana. Nimekataa kabisa. Uliniudhi ulipoacha kanisa langu kwa dharau na sasa umerudi kudai unataka kumposa binti yangu,” mzee aliwaka.

Kila mtu alishangaa huku wakimtazama jamaa kwa huruma. Mzee alipozusha zaidi, jamaa aliondoka na kwenda zake akifuatwa na marafiki zake.

  • Tags

You can share this post!

Kanisa latetea Oburu kushiriki sakramenti

Atwoli sasa agutuka kuhusu gharama ya maisha

T L