NA RICHARD MUNGUTI
MUME aliyemchapa mke waliyetengana ameshtakiwa mahakamani.
Jaylan Mwaniki alishtakiwa mbele ya hakimu mwandamizi Derrick Kutto kwa kumshambulia na kumuumiza Barbra Vugutsa katika kijiji cha Mathonge eneo la Waithaka kaunti ya Nairobi mnamo Machi 14.
Hakimu alifahamishwa kisa hicho kilitokea mwendo wa saa 11 alfajiri.
Mshtakiwa alimshambulia Vugutsa alfajiri alipofungua nyumba na kumpata akimvizia nje ya nyumba.
Mshtakiwa aliingia ndani ya nyumba na kuanza kumnyeshea makonde na masumbwi.
Vugutsa aliponyoka na kutoroka lakini Mwaniki akamfuata unyounyo.
Wananchi walimwokoa Vugutsa.
Mahakama ilimwachilia mshtakiwa kwa dhamana ya pesa taslimu Sh20,000.