Na RICHARD MUNGUTI
MSHUKIWA wa ujambazi ameshtakiwa kwa wizi wa kimabavu baada ya kupatikana akiwa na baiskeli iliyoporwa na wahuni.
Victor Ochieng alishtakiwa mbele ya hakimu mkazi Eric Mutunga.
Ochieng alidaiwa alimnyang’anya Samson Radier baiskeli katika eneo la Darfur mtaa wa Kariobangi North mnamo Mei 2, 2023.
Radier alishambuliwa na kundi la vijana akielekea nyumbani na kunyang’anywa simu ya kiungambali, baiskeli, kitambulisho na kifaa cha maji zote za thamani ya Sh28, 999.
Wakati wa kisa hicho Radier aliumizwa.
Mshtakiwa pia anakabiliwa na shtaka la kupatikana na mali iliyoibwa au kupatikana kwa njia isiyo halali.
Ochieng alikana mashtaka dhidi yake.
Kesi hiyo itasikizwa Septemba 18, 2023.