NA RICHARD MUNGTI
MPENZI amezuiliwa rumande na polisi kwa tuhuma za kumuua ‘babe’ wake baada ya kuishi pamoja kwa wiki moja.
Simon Masafu Omoyo anadhaniwa alimuua Esther Nyamache Sebe aliyekuwa na umri wa miaka 19.
Nyamache alikata roho katika hospitali ya Eagle iliyoko mtaani Dagoretti.
Mwili wake ulikuwa na majeraha.
Madaktari kwenye hospitali hiyo waliwaita polisi baada ya kushuku Nyamache alipigwa na kuumizwa na Omoyo kabla ya kumpeleka hospitali.
Nyamache alikutana na Omoyo baada ya kufanya mtihani wa Darasa la Nane.
Baada ya kutumiana jumbe za mapenzi, Nyamache aliondoka nyumbani kwao Kisii na kuanza kuishi na Omoyo katika eneo la Gathondeki mtaani Kawangware jijini Nairobi.
Marehemu aliishi na Omoyo kati ya Desemba 5 hadi Desemba 14 alipoaga dunia kwa njia tata.
Hakimu mwandamizi Charles Mwaniki aliamuru mshukiwa huyo azuiliwe kwa siku saba kabla ya kushtakiwa kwa mauaji ya Esther Nyamache Sebe.