• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 3:16 PM
Baba azuiliwa kwa madai ya kupiga na kuua bintiye aliyeshiriki mapenzi

Baba azuiliwa kwa madai ya kupiga na kuua bintiye aliyeshiriki mapenzi

NA VITALIS KIMUTAI

POLISI wanachunguza kisa ambapo mwanafunzi wa kike alifariki akitibiwa hospitalini baada ya kuadhibiwa kwa kupigwa kwa mbao na baba yake mzazi.

Naomi Chelangat, 16, mwanafunzi wa Kidato cha Pili alipata kipigo kutoka kwa baba yake, Isaiah Kibet Sawe, 44, baba wa watoto watatu, ambaye anazuiliwa na polisi akisubiri kufikishwa kortini.

Inadaiwa kwamba mzee Sawe alikasirika baada ya kaka zake Chelangat kumuarifu kwamba dada yao alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na mwanamume mmoja wa kijijini kwao.

Chelangat alikimbizwa hospitalini Septemba 23, na alikuwa akitibiwa majeraha mabaya ya ndani kutokana na kichapo.

Chelangat, mwanafunzi wa zamani katika shule ya upili ya Sagamian Kaunti ya Narok alidai kabla ya kufariki kuwa kaka zake – ambao aliwasamehe – walikuwa wamemjulisha babake kuhusu madai ya uhusiano na mwanamume huyo kutoka mtaani kwao.

Kulingana na ripoti ya polisi, msaidizi wa chifu eneo ndogo la Tendwet, Daniel Kones aliripoti kwamba Chelangat alipigwa Septemba 23 katika kijiji cha Jerusalem.

Kufuatia kifo hicho, babake Chelangat alikamatwa na polisi na anatarajiwa kufikishwa mahakamani kushtakiwa kwa mauaji.

Aliokolewa na polisi kutokana na ghadhabu za wananchi baada ya habari kuenea kuwa msichana huyo aliaga dunia kutokana na majeraha aliyoyapata.

“Ni kweli sisi (polisi) tunazuilia mshukiwa kabla ya kufikishwa mahakamani. Alizuiliwa katika kituo cha polisi cha Tendwet kabla ya kuhamishwa hadi Narok ili ndiposa afikishwe mahakamani,” afisa mmoja asiyeruhusiwa kuzungumza na wanahabari akadokeza.

Binti Chelangat alisaidiwa na majirani kutoka kijini kumpeleka katika hospitali ya Rufaa iliyo katika kaunti jirani ya Bomet.

“Tulimpata amezimia baada ya babake kumpiga, akamvuta na kumtupa ndani ya chumba chake cha kulala kabla ya sisi kumkimbiza hospitalini,” Bw Eliud Kirui akasema.

  • Tags

You can share this post!

Ugaidi: Familia yataka jamaa arudishwe nchini

Demu aanika siri za ndoa yake, rafiki yake apindua ajenda...

T L