NA FARHIYA HUSSEIN
SERIKALI ya Kaunti ya Mombasa inawania kuanzisha mbinu ya wakazi na wagonjwa wanaohudumiwa katika Hospitali Kuu ya Pwani almaarufu Coast General kupeleka malalamishi yao moja kwa moja, suala ambalo linatarajiwa kupunguza visa vya kudhulumiwa katika hospitali hiyo.
Hii ni baada ya wakazi na wagonjwa kutoa malalamishi yao mara kadhaa kuhusu huduma duni wanazopokea katika hospitali ya Coast General.
Kulingana na wakazi wa Pwani, hili limekuwa donda sugu kwa miaka kadhaa, wengi wakilaumu wahudumu wa hospitali hiyo kwa kuwadhulumu.
Katika video ya hivi majuzi iliyozua gumzo mtandaoni, mwanamume mmoja alionekana akilalamika jinsi mgonjwa wake aliyekuwa amemleta kutoka kaunti jirani ya Kilifi ili kupokea matibabu katika hospitali hiyo alivyodhulumiwa.
Video hiyo ilionyesha akimuuliza daktari mmoja wa hospitali hiyo, akitaka kuelezwa ni kwa nini mgonjwa wake alikuwa bado kushughulikiwa.
Aidha, Kaunti ya Mombasa sasa inatarajia kuziba pengo hilo kwa kufungua laini ya mawasiliano ambapo mgonjwa au mlalamishi ataweza kutuma lawama zake moja kwa moja kwa afisi zao.
Mpango huo pia unapania kuwatuza wahudumu watakaonekana wakifanya kazi yao vyema.