NA ALEX KALAMA
SERIKALI ya Kaunti ya Kilifi imeombwa kunakili stakabadhi rasmi za umma kwa Kiswahili ili kufikia idadi kubwa ya wananchi.
Wanaharakati katika kaunti hiyo walilalamika kuwa, wengi wa wakazi hawaelewi mipango ya kaunti kwa vile stakabadhi huandikwa kwa Kiingereza ambacho ni kigumu kwao kuelewa.
Vilevile, hali hiyo imedaiwa kuchangia wengi kutohudhuria vikao vya umma kujadili mipango ya kaunti.
Mwanaharakati wa kutetea haki za watoto na wanawake katika kaunti hiyo, Bi Hilder Lameck, alisisitiza haja ya nakala hizo kuchapishwa kwa lugha ya Kiswahili.
Wakizungumza katika kikao kilichoandaliwa na shirika la Kilifi Citizen Forum na pia kilichowahusisha maafisa wa serikali ya kaunti ya Kilifi, wamesema kuwa iwapo nakala zitachapishwa kwa lugha ya Kiswalihi, kila mwananchi atafahamu kile kinachoendelezwa na serikali ya kaunti.
“Ni wanawake wachache ambao huwa wanahudhuria vikao vya umma. Tumeona hizi nakala nyingi zinaandikwa uzungu mwingi, na kuna kina mama wengine hawajasoma, wengine wamesoma kwa uchache. Tunaomba hizi nakala kuandikwa kwa lugha ya Kiswahili ili kutoa nafasi kwa kila mwananchi kutoa maoni yake katika vikao hivi. Na ziletwe kwa Kiswahili ambacho kila mtu anaweza kusoma na kuelewa kwa urahisi, wasitumie maneno magumu magumu,” akasema Bi Lameck.
Kwa upande wake, kiongozi wa watu wanaoishi na ulemavu katika eneo la Malindi, Bw Emmanuel Ogutu, alitaka sheria ya kujumuisha walemavu katika shughuli zote za kiserikali itekelezwe kikamilifu.
Subscribe our newsletter to stay updated