• Nairobi
  • Last Updated May 11th, 2024 7:15 PM
Kundi la Malenga Wamilisi na Kiswahili ni chanda na pete

Kundi la Malenga Wamilisi na Kiswahili ni chanda na pete

KUNDI la Malenga Wamilisi linajumuisha watunzi wa mashairi wenye umilisi katika utanzu huu wa fasihi.

Kwa mujibu wa Mtaala Mpya wa Umilisi (CBC), ni muhimu kwa waandishi kuegemeza kazi zao bunilizi katika mkondoelimu huo.Kundi hili lilibuniwa Februari 14 mwaka huu huku waanzilishi wakiwa ni Elisha Otoyi, Momanyi Henry Rioba, Alfred Lobawoi na Timothy Omusikoyo Sumba.

Pindi tu lilipozaliwa, wafuasi chungu nzima walifurika kundini nao wakawaleta ndugu, jamaa, majirani na marafiki.Wingi huo wa washairi ulilipa kundi uthabiti wa hali ya juu na bado linazidi kukita mizizi, kustawi na kunawiri.

Ama kweli elfu huanza na moja!Sawa na makundi mengine ya kupigia Kiswahili chapuo, kundi hili nalo linalenga kukuza vipaji vya watunzi na waandishi chipukizi na kuwaboresha wale waliobobea.Linaazimia pia kutunga na kuandika diwani za ushairi, hadithi za umilisi (kwa watoto), riwaya, tamthilia na hadithi fupi.

Madhumuni mengine ya kundi hili linalojivunia wanachama 108 kufikia sasa, ni kukitetea Kiswahili nchini Kenya na kuchangia makuzi yake kote ulimwenguni.Katika kundi hili, kinachopewa kipaumbele ni masomo na mafunzo belele. Isitoshe, watunzi hupakia mashairi yao kwenye kundi la mtandaoni la Malenga Wamilisi ili kuburudisha na kufunza wenzao.

Masuala ibuka yanayogonga vichwa vya habari katika sekta ya elimu pia hujadiliwa kundini kwa sababu robo tatu ya wanachama ni walimu na wanataaluma mbalimbali wanaojihusisha na masuala ya elimu kwa namna moja au nyingine.

Kundi hili pia ni ukumbi wa maswali mwafaka ambayo hujibiwa papo kwa hapo na wanachama. Mizaha na utani pia hupenyezwa kiasi fulani. Hakuna dawa nzuri kuliko kichekesho!Licha ya kubuniwa majuzi, kundi hili limefanikiwa pakubwa. Wanachama tayari wamefyatua diwani kadhaa za mashairi huku mchakato wa kukusanya hadithi fupi ukiendelea.

Baadhi ya kazi za kundi hili ambazo tayari zimechapishwa ni: Malenga wa Afrika, Wosia na Mashairi Mengine, Malenga wa Kenya (Gredi ya 1, 2, 3), Malenga wa Kenya (Gredi ya 4, 5, 6), Tasnia ya Ushairi, Wasifu wa Timothy Sumba na Game of Wits (Antholojia ya Kiingereza).

Baadhi ya wanachama ni Dkt Beverlyne Asiko Ambuyo (Chuo Kikuu cha Maseno), Dkt Jackline Njeri Murimi (Chuo Kikuu cha Tom Mboya) na Fatma Ali Mohamed (Zanzibar).Wengine ni Tabitha Mawia Manzi, Collins Ochieng, Fatma Suleiman Salim (Zanzibar), Gakurya Mwinyi wa Lebanon, Wambugu Yusuf ambaye ni mhariri wa Kiswahili TV 47, mwanahabari Andrine Kilemi (TV 47) na Timothy Omusikoyo Sumba ambaye ni mlezi mkuu wa kundi.

  • Tags

You can share this post!

Shule ziboreshwe ili kuepusha ushindani mkali uliopo kwa...

Papara na pupa hazileti ufanisi katika maisha