• Nairobi
  • Last Updated May 12th, 2024 10:50 AM
Maafisa wawasaka majambazi walioua mfanyabiashara mtaani

Maafisa wawasaka majambazi walioua mfanyabiashara mtaani

Na Sammy Kimatu

WANAUME wawili walipigwa risasi na washukiwa wa ujambazi katika mtaa mabanda, tarafa ya South B katika kaunti ndogo ya Starehe.

Aidha, mtu mmoja alifariki papo hapo naye wa pili akiuguza majeraha katika hospitali ya Rufaa ya Kenyatta alikolazwa.Kisa hiki kilitokea katika mtaa wa mabanda wa Mukuru-Fuata Nyayo, wadi ya Nairobi Kusini dakika chache kasoro saa nne za usiku.

Mkuu wa Polisi eneo la Makadara, Bw Tim Odingo alisema aliyefariki alikuwa mfanyabiashara aliyepatwa na majambazi alipokuwa akifunga duka lake.Mbali na hayo, Bw Odingo alisema kundi la vijana wanne waliingia mtaani humo wakiimba ‘polisi’, ‘polisi’ na ndipo pakazuka mguu niponye kwa wakazi waliokuwa barabarani wakidhania labda polisi wamefika kuwakamata wanaopuuza saa za kafyu.

Katika kukurukakara hizo, majambazi walipora simu za watu huku mama mmoja aliyekuwa akiuza kuku waliochemshwa, akiibiwa chakula hicho. “Majambazi walipiga nduru wakisema polisi, polisi ndiposa watu wakaanza kukimbia wakifikiria kuna msako wa polisi wa kutekeleza kafyu,” Bw Odingo akasema.

Bali na hayo, majambazi hao walimpata mwanabiashara mwingine akifunga mlango wa duka lake na kumwamuru awapatie pesa.Hata hivyo, mwenye duka alidinda kutii amri yao na ndipo alipokuwa aking’ang’ana na jambazi mmoja, mshukiwa wa pili aliyekuwa upande wa nje ya duka akachomoa bastola na kumfyatulia risasi moja iliyompata na kumuua papo hapo.

Huku wakitoroka, majambazi hao walifyatua risasi nyingine ambayo kwa bahati mbaya ilipata mkazi mmoja na kumjeruhi.Aliyejeruhiwa alikimbizwa hospitalini ya rufaa ya Kenyatta anakoendelea na matibabu.

Polisi waliokuwa wakishika doria katika barabara ya Aoko walifika upesi katika eneo la kisa baada ya kusikia milio ya risasi na kupata mwili wa mwanamume aliyeuawa karibu na duka lake.Kadhalika, Bw Odingo alidokeza kwamba maafisa wa polisi walipata risasi moja na ganda la risasi iliyotumika katika eneo la mkasa.

Hata hivyo haikujulikana kama kuna pesa zozote ambazo ziliibwa kutoka kwa duka la aliyeuliwa.Vilevile, aliongeza kwamba washukiwa walitorokea ndani ya mtaa wa mabanda wa Kayaba na kuongeza kwamba maafisa wake wamo mbioni kuwasaka washukiwa wote wanne wanaoaminiwa hujificha mtaani wa Kayaba.

“Tumeanzisha msako mkali ili tuwakamate waliohusika na kitendo hicho baada ya kupata habari zitakazotuelekeza kuwakamata washukiwa wote wanne,” Bw Odingo asema.Kwa muda mrefu, usalama katika mitaa ya mabanda ya maeneo ya South B, Eneo la Viwandani, Lunga Lunga na mtaa wa Kwa Reuben umeimarika baada ya kambi zaidi za polisi kuongezwa mitaani.

“Usalama katika eneo la Makadara umeimarika pakubwa kwani hakukuwa na visa vya majambazi walkiojihami kuvamia wananchi katika siku za hivi karibuni baada ya kuongeza kambi za polisi mashinani,” Bw Odingo akanena

  • Tags

You can share this post!

Ni Gor na Wazito huku nao Tusker wakitazama meza

Kijana ajeruhiwa baada ya kushambuliwa na kiboko