• Nairobi
  • Last Updated May 11th, 2024 1:12 PM
Ni Gor na Wazito huku nao Tusker wakitazama meza

Ni Gor na Wazito huku nao Tusker wakitazama meza

FATAKI zinatarajiwa leo katika uga wa Thika, mibabe Gor Mahia wakitifua vumbi dhidi ya mabwenyenye Wazito katika mechi kali ya Ligi Kuu.

Tayari pande zote zimeanza kujipiga kifua na kuzua mihemko kabla ya mtanange huo huku kiungo wa Wazito Kevin Kimani akisema timu hiyo haiwezi kukubali kulazwa kwa mara ya pili na Gor.Katika mechi nyingine, mabingwa mara 13 AFC Leopards nao wana kibarua kigumu dhidi ya wavutamkia Mathare United kuanzia saa tisa na robo ugani Ruaraka.

Nambari mbili Tusker nao watamaliza udhia dhidi ya Western Stima katika uga huo huo kwenye mechi ya mapema itakayoanza saa saba mchana.K’Ogalo ilibwaga Wazito 1-0 katika mchuano wa mkondo wa kwanza na Kimani anasema mara hii wapo tayari kulipiza kisasi na kujizolea alama zote tatu muhimu.

Katika mechi kati ya Gor na ‘masonko’ hao iliyosakatwa mnamo Mei 31, bao la Jules Ulimwengu la dakika ya 82 lilitosha kuipa K’Ogalo ushindi licha ya Wazito kumiliki asilimia kubwa ya mpira katika kipute hicho.

‘Hatuwezi kuwaruhusu watuchape mara mbili. Mara hii haitakuwa mechi rahisi na hakuna mteremko. Lazima tulipize kisasi na kuwapiga ili nasi tupande juu kwenye jedwali,’ akasema Kimani wakati wa mahojiano na Taifa Leo.

Mvamizi wa zamani wa K’Ogalo Boniface Omondi ambaye kwa sasa anasakatia Wazito, naye alisema hakutakuwa na huruma kwa timu yake ya zamani.’Hapa ni kazi tu na kwa kuwa walitushindia pembamba katika mkondo wa kwanza, lazima tulipize kisasi.

Tutapigania ushindi kwa jino na ukucha wala sitajali kuwa walikuwa waajiri wangu zamani,’ akasema Omondi aliyeondoka Gor mnamo Septemba mwaka jana kutokana na njaa baada ya kukosa mishahara ya miezi kadhaa.

Hata hivyo, winga wa Gor Clifftone Miheso naye alieleza Taifa Leo kuwa hawapo tayari kupoteza dhidi ya Wazito hasa wakati huu ambapo wako pazuri kutwaa taji la ligi.

Kujikakamua

‘Kila timu hujikaza sana ikicheza dhidi ya Gor na mechi ya Wazito haitakuwa tofauti. Sisi tunalenga taji na hatuko tayari kuachilia mkondo mzuri wa ushindi katika mechi saba mfululizo kuvurugwa,’ akasema Miheso.

Huku Gor wakiwa katika nafasi ya tatu kwa alama 37 baada ya kujibwaga uwanjani mara 19, Wazito wapo nambari 10 kwa alama 26 na ushindi utawapaisha hadi nafasi ya sita kwa alama 29 jedwalini.Tusker nayo itaiondoa KCB kileleni mwa jedwali iwapo itaishinda Western Stima.

Wanamvinyo hao wana alama 41, mbili tu nyuma ya KCB.Aidha, kocha wa Mathare United Frank Ouna atalenga ushindi wake wa kwanza iwapo vijana wake wataichapa Leopards.

  • Tags

You can share this post!

Rais kuzindua Safari Rally ulinzi mkali ukiwekwa

Maafisa wawasaka majambazi walioua mfanyabiashara mtaani