Siku hizi mwanasiasa huyo ambaye alikwea ngazi kutokana na sarakasi zake nyingi, ana upweke mwingi japo anasema kuwa anapanga kurejea kwa kishindo katika uchaguzi mkuu wa 2027, akilenga kiti cha eneobunge hilo. Akizungumza katika eneobunge la Seme mnamo Jumamosi wakati wa mazishi ya Mama Hilda Okethi, mfanyabiashara ambaye alikuwa kati ya wafuasi wake kindakindaki, Bw Ouda alifichua kwamba siasa zilimtumbukiza kwenye madeni na sasa amesalia ‘hana kitu’.
“Najua jinsi ambavyo nilikuwa naumia mfukoni na mahali ambapo nilikuwa napokea mikopo ili kuhakikisha kwamba kampeni zangu ni dhabiti. Ilifikia mahali ambapo marafiki zangu walinihepa na nikasalia na mwananchi wa kawaida,” akasema Bw Ouda.
“Ni mimi ndiye nilijua mzigo ambao nilikuwa nimebebeshwa na jinsi nilivyoumia. Hakuna aliyejua zaidi yangu jinsi ambavyo pesa ziliniishia wakati wa kampeni mpaka nikakopa,” akaongeza. Kinyume na baadhi ya wanasiasa ambao walielekea kortini baada ya kushindwa uchaguzini, hali ilikuwa tofauti kwa Bw Ouda ambaye anasema aliishiwa na hakuwa na pesa za kupinga ushindi huo.
“Hiyo ndiyo maana siku hizi unaona nimekimya sana. Watu wameniacha na nimekubali hali yangu. Kile nimebaki nacho ni Mungu wangu,” akasema Bw Ouda.
Wakati ambapo baadhi ya wanasiasa kutoka eneo la Nyanza wanakimbilia kambi ya Rais William Ruto, Bw Ouda naye anasema hawezi kumhepa Kinara wa ODM Raila Odinga na ataendelea kumuunga mkono akisubiri uchaguzi wa 2027.
“Mamako anaweza kukuchapa au kukuadhibu vibaya mpaka umlaani na utishie kutorokea kwa mama mwengine. Hata hivyo, kabla sijafanya hivyo, huwa najiuliza ni nini napitia au manufaa nitakayoyapata kutoka kwa mama wa kambo ambayo siwezi kupata kwa mamangu?” anauliza.