NA IRENE MUGO
MBUNGE wa Kieni, Kanini Kega amemkosoa Naibu Rais William Ruto kwa kile amesema ni kukosoa serikali akiwa ndani yake.
“Amekuwa akidai alichangia kufaulu kwa miradi ya serikali ilhali anaikosoa akisema imeshindwa katika ajenda zake,” Bw Kega alisema Jumatatu.
Mnamo Jumapili, Rais Uhuru Kenyatta na Dkt Ruto walinyoosheana kidole cha lawama kila mmoja akikosoa mwingine kufuatia tofauti zao.
Bw Kega, ambaye amekuwa mshirika wa karibu wa Rais Kenyatta, alisema ana uhakika kuwa muungano wa Azimio la Umoja One Kenya utashinda viti vingi vya ubunge, useneta na ugavana kwenye uchaguzi mkuu wa Agosti 9.
Bw Kega alisema Dkt Ruto anafaa kuwa mtu wa mwisho kulaumu serikali inayomlipa mshahara.
Kwenye hotuba yake alipokuwa akihutubu kuadhimisha Leba Dei mnamo Jumapili, Rais Kenyatta alimwambia Dkt Ruto ajiuzulu akisema hamsaidii kwa chochote katika kusimamia serikali.
Dkt Ruto naye alijibu akisema iwapo rais anataka wasaidiane kutatua shida za Wakenya yuko tayari kufanya hivyo iwapo ataombwa kusaidia.