Na RICHARD MUNGUTI
RAFIKIYE mfanyabiashara aliyeuawa kinyama katika eneo la Kilimani Nairobi alitembelewa na wanaume wawili usiku huo.
Mmoja wa wanaume hao alisemekana kuwa “mlinzi katika Ikulu ya Nairobi.”Akitoa ushahidi mbele ya Jaji Grace Nzioka, Bw Antony Kaka alisema pia alimtembelea Monicah Kimani usiku huo wa Septemba 19 2018 lakini,walikutana kwenye lango kuu la kuingia mtaani humo.
Alisema Monicah alimweleza alikuwa na wanaume wawili waliokuwa wamemtembelea, mmoja raia wa Lebanon na mwingine “Mlinzi katika Ikulu.”Bw Kaka alisema hayo alipotoa ushahidi dhidi ya Joseph Irungu almaarufu Jowie na aliyekuwa mtangazaji Jackie Maribe walioshtakiwa kwa mauaji ya Monicah usiku wa Septemba 19/20 2018.
“Nilipowasili katika makazi hayo mwendo wa saa tatu unusu usiku, Monicah alitoka kwake tukakutana kwenye lango kuu.Tulikumbatiana kisha akanieleza alikuwa na wageni wawili mmoja raia wa Lebanon na mwingine Afisa wa Ulinzi katika Ikulu,” alisema Bw Kaka.
Baadaye usiku huo mwendo was aa tano usiku Monicah alimtumia ujumbe “akimtaka aende akamsaidie kulala.”Alisema aliupokea ujumbe huo maalum na wa kipekee kutoka kwa Monicah.
“Je ulijibu ujumbe huo,” wakili Prof Hassan Nandwa alimwuliza Bw Kaka.“Ndio nilimjibu kwamba nitaenda keshoye Septemba 20 2018,” Kaka alijibu.Hata hivyo , Bw Kaka alieleza korti alimpigia Monicah simu lakini hakuzipokea.
Hatimaye alipokea habari kwamba Monicah aliaga.Shahidi huyo alikanusha madai ya Prof Nandwa kwamba yeye na Monicah walikuwa wapenzi.Bw Kaka alikataa kata walikuwa wapenzi na marehemu ila alidumisha “walikuwa marafiki tu wa kawaida.”
Bw Kaka alisomewa ushahidi wa Bw Owen aliotoa kortini akisema “usiku wa Septemba 19, 2018 alimtembelea Monicah alipowasili kutoka Sudan kusini alipokuwa akifanya biashara na kumpata Walidi na mwanaume mwingine aliyeelezwa na Monicah, Jowie ni afisa wa polisi wa kimataifa (Interpol).”
Mwendo wa saa nne kasorobo Walidi alitoka kwa Monicah na kumwacha Jowie.Mashahidi waliowatangulia Mabw Kaka na Owen walimweleza Jaji James Wakiaga aliyekuwa akisikiza kesi hiyo, walisema Jowie aliachwa akiwa na Monicah.
Mwili wa Monicah ulikutwa umefungwa ukiwa na majeraha na kutupwa ndani ya karai.Jowie na Maribe wamekanusha walimuua Monicah. Wako nje kwa dhamana.
Kesi inaendelea.