• Nairobi
  • Last Updated May 21st, 2024 8:55 PM
Mishi Mboko aongoza kurusha ndoano mtandaoni kusajili wafuasi wa ODM

Mishi Mboko aongoza kurusha ndoano mtandaoni kusajili wafuasi wa ODM

NA WINNIE ATIENO

WABUNGE wa ODM eneo la Pwani wakiongozwa na Bi Mishi Mboko (Likoni), Bi Amina Mnyazi (Malindi), na Mwakilishi wa Wanawake Kaunti ya Mombasa Bi Zamzam Mohammed wameanza kusajili wanachama wa ODM mtandaoni.

Viongozi hao walisema wameanza zoezi hilo baada ya kinara wao wa chama Bw Raila Odinga kuzindua usajili wa wanachama.

Bi Mboko na Bi Mohammed wamewasihi wakazi wa Mombasa kujiandikisha kama wanachama wa ODM ili kuongeza idadi yao, huku wakirusha ndoano kwenye mtandao ya kijamii kusaka ufuasi.

Akiongea mtandaoni, Bi Mboko alisema chama cha ODM kina lengo la kuwakomboa Wakenya kutokana na udhalimu.

“Ninawaomba mujisajili na uwe mwanachama halisi wa ODM. Wale ambao ni wanachama watathmini kama bado ni wanachama wa ODM. Nendeni kwenye mtandao wa chama cheti mujiandikishe. Wingi wetu ni msingi thabiti, tujiandikishe kama wanachama wa ODM ili tuweze kupigana na minyororo ya hali ngumu ya maisha,”  alisema Bi Mboko.

Mbunge huyo ambaye ni mwanamke pekee aliyeshinda ubunge, aliwasihi wanawake kujitokeza kwenye siasa ili kubadilisha mkondo wa siasa nchini.

“Hiki ni chama ambacho tunajivunia. Jisalili katika chama chetu, tuweze kupeleka uchumi wa Kenya mbele na tushirikiane kujenga taifa letu kwa pamoja. Hakuna chama kingine,” alisema Bi Mohammed akimtaja Bw Odinga kama mtetezi wa wanyonge.

Naye Spika wa Bunge la Kilifi, Bw Teddy Mwambire aliwasihi wakazi kujiandikisha kama wanachama wa ODM.

“Ninawasihi viongozi wa ODM wahamasishe umma kuhusu zoezi hili la kitaifa ili tupate uungwaji mkono na umaarufu wa chama. Serikali ya Kenya Kwanza imekumbwa na shutuma chungu nzima za ufisadi,” alisema.

Haya yanajiri wiki moja baada ya Kinara wa ODM, Bw Raila Odinga kuzindua zoezi la kusaka wanachama nchini.

 

  • Tags

You can share this post!

Gachagua na Gavana Nassir wakabana koo kuhusu pesa za El...

Mgeni aliye na mashtaka saba ya kunajisi watoto amjibu jaji...

T L