SHANGAZI;
Mpenzi wangu amekuwa akinisaidia kulea mtoto tuliyezaa pamoja. Aliachishwa kazi mapema mwaka huu anataka tuachane kwa sababu hana uwezo wa kunisadia. Ananiambia nitafute mwanamume mwingine. Nimechanganyikiwa, nishauri.
Ni jambo la kushangaza kwamba mwanamume uliyemzalia akidai kukupenda sasa anakwambia utafute mwingine ili akusaidie kulea mtoto wenu. Hiyo ina maana kwamba utabeba mzigo huo peke yako kwani na huwezi kumlazimisha.
Niliingia katika uhusiano wa kimapenzi na mwanamume ambaye sikuwa na hisia kwake nikidhani hatimaye ningempenda. Huu ni mwaka wa pili na moyo umemkataa. Nifanyeje?
Huo ni ulaghai wa kimapenzi. Ulimhadaa mwanamume huyo kuwa unampenda na atavunjika moyo sana akijua huna hisia kwake. Usiendelee kumpotezea wakati. Mwambie ukweli ili muachane atafute mwingine.
Huu ndio mwaka wangu wa pili katika uhusiano wa kimapenzi. Nimefikiria sana kuhusu mwanamume niliye naye kugundua nimepoteza wakati wangu bure kwani sijaona lolote la maana kwake. Nishauri.
Msimamo wako ni kuwa humpendi mwanamume huyo na hutaki kuendelea na uhusiano huo. Usipoteze wakati zaidi, ukweli huo ili muachane kila mmoja wenu aendelee na maisha yake.
Nina mpenzi na ninampenda kwa dhati. Nimekuwa nikijitolea kwa ajili yake kila anaponihitaji. Lakini nikimhitaji kimahaba hunihepa kupitia vijisababu. Nahisi kuwa hanipendi. Nishauri.
Wapenzi wa dhati wanafaa kusaidiana kwa kila hali. Kama mpenzi wako akikuhitaji huwa unapatikana ili kumfaa, inafaa kuwa hivyo kwake. Tabia yake hiyo ni dalili kuwa hakupendi. Kama unahisi hakupendi achana naye.