Na LABAAN SHABAAN
Makachero wa Idara ya Ujasusi wa Jinai (DCI) wamepata mavazi yanayoaminiwa kuvaliwa na mshukiwa mkuu wa mauaji ya kikatili ya Kaimu Mkurugenzi wa Fedha katika Hospitali ya Nairobi Bw Eric Maigo Ijumaa iliyopita Septemba 15, 2023.
Haya yanajiri siku moja baada ya DCI kuchapisha picha za mshukiwa huyo mitandaoni ikiomba wakenya watoe ripoti kumtambua ili atiwe mbaroni.
Mavazi hayo, shati lenye alama mraba nyekundu na suruali ya kijivu yenye chapa za wanyama, yalipatikana katika nyumba ya mbao Kijiji cha Bombolulu katika mtaa wa Kibera jijini Nairobi.
Mshukiwa huyo ambaye majasusi wamemtambua kwa jina Bi Ann Adhiambo anayejulikana kwa lakabu ya “Nut”, yuko mafichoni na bado mkono mrefu wa serikali haujamfikia.
DCI inadokeza kuwa Bi Adhiambo angali mtoto kwa sababu anaaminiwa kuwa na umri wa miaka kati ya 15 na 17.
Wapelelezi kadhalika wanafichua kuwa huenda mtuhumiwa ana rekodi ya uhalifu kwa sababu alifanya Mtihani wa Kitaifa wa Shule ya Msingi (KCPE) kati ya mwaka wa 2021 na 2022 katika shule inayosajili watoto wahalifu ya Dagoretti Approved School.
Makachero wanaendelea kuomba raia watoe ripoti inayoweza kusaidia kukamatwa kwa “Nut” na kuwasilisha katika kituo chochote cha polisi.
Picha za kamera za usalama za CCTV zinaonyesha msichana huyo akiruka ukuta wenye seng’enge baada ya ‘kutekeleza mauaji’ usiku wa manane katika makazi ya Bw Maigo Woodley Annex – Upper jijini Nairobi.