Na RICHARD MUNGUTI
BINTI aliyemtukana baba yake matusi nyeusi kabla ya kuwafungia nje ya makazi yao jijini Nairobi amefikishwa kortini.
Faith Mokeira alishtakiwa kwa kuzua vurugu na kuhatarisha amani.
Alishtakiwa kwa kuwafungia nje wazazi wake, David Nyambane na mkewe.
Hata hivyo, alikana shtaka linalomkabili.
Ilibidi wazazi hao waombe malazi kwa jirani kwa vile Mokeira alikuwa amewanyima raha ya kulala raha mustarehe katika boma lao mtaani Kasarani, Nairobi.
Kisa hicho, Hakimu Mkuu Francis Kyambia alifahamishwa kilitokea katika eneo la Marurui, Kasarani mnamo Mei 8, 2023.
Aidha, ilibidi polisi watumie mbinu mwafaka kumtimua Mokeira ndani ya nyumba hiyo.
Mbali na kuwafungia wazazi wake nje, Mokeira alimwangushia baba yake matusi meusi tusiyoweza kuyachapisha.
Mshtakiwa aliachiliwa kwa dhamana ya Sh4, 000.
Kesi hiyo itatajwa Mei 29, 2023 kutengewa siku ya kusikizwa.