• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 6:55 PM
Mumewe mbunge amlaumu Ruto vikali

Mumewe mbunge amlaumu Ruto vikali

Na STANLEY NGOTHO

MUME wa mbunge wa Kajiado Mashariki, Peris Tobiko, Bw Kishanto Ole Suuji, amemlaumu Naibu Rais William Ruto kwa kufanyia mkutano katika boma lake bila idhini yake.

Bw Suuji alimshutumu Ruto kwa kupanga mkutano wa kisiasa na mkewe bila kumwarifu.

Mkutano huu ulifanyika nyumbani kwake IIporosat, kaunti ndogo ya Kajiadio Mashariki.Bw Suuji alisema kuwa alikasirishwa na njama ya kuwaleta wajumbe nyumbani kwake bila ya kumwarifu.

Ijumaa, Bw Ruto alikuwa nyumbani kwa Bi Tobiko kwa mkutano ambao ungemwezesha Bi Tobiko kuhamia chama cha United Democratic Alliance kutoka Jubilee.

Wanasiasa wanaounga mkono UDA walisafirishwa nyumbani kwake Bi Tobiko kuanzia saa moja asubuhi.

Wajumbe pamoja na Naibu Rais walipokuwa wakiwasili nyumbani kwao, Bw Suuji alikuwa akizunguka kwenye vituo vya polisi ili kulalamikia ‘njama’ ya mkewe na Ruto.

Bw Suuji alikutana na Bi Ancent Kaloki, Mkuu wa Polisi (OCPD) Isinya, kabla ya kuhutubia wanahabari kumlaumu mkewe na Naibu Rais.

“Walivamia nyumba yangu bila kunifahamisha. Wameharibu mimea yangu na kuwachinja mifugo wa familia yangu. Nimesikitika sana,” akasema Bw Suuji.

Bw Suuji ambaye ni Kamishna katika Tume ya Ugavi wa Mapato (CRA) alisema kuwa yeye kama afisa wa serikali hafai kuwa na mkutano kama huo nyumbani kwake.

Bw Suuji ambaye anaunga azima ya urais ya kiongozi wa ODM, Raila Odinga, alitishia kumshtaki Naibu Rais na mbunge Tobiko kwa kuvamia nyumba yake.

Mkutano huo wa IIpolosat unatamatisha mvutano kati ya Bi Tobiko na mbunge wa Kajiado Kusini, Katoo Ole Metito ambaye alikuwa akimezea mate tikiti ya UDA.

Washauri wa Naibu Rais walimshauri kutomuunga mkono Bw Metito na badala yake akumbatie Bi Tobiko kugombea ugavana ili aweze kumenyana na gavana wa sasa Joseph Ole Lenku kwenye uchaguzi mkuu ujao.

You can share this post!

TANZIA: Mtangazaji Badi Muhsin afariki

Kobia ataka maafisa waadilifu NGEC