• Nairobi
  • Last Updated May 12th, 2024 8:50 AM
Muungano wa kisiasa wa kaunti za Mashariki pigo kwa Mlima Kenya

Muungano wa kisiasa wa kaunti za Mashariki pigo kwa Mlima Kenya

Na BENSON MATHEKA

HUENDA eneo la Mlima Kenya likakosa nguvu za kisiasa ambazo limekuwa likijivunia ikiwa juhudi za kuunganisha kaunti nane za uliokuwa mkoa wa Mashariki zitafaulu.

Tayari baadhi ya wanasiasa kutoka kaunti hizo wanataka eneo hilo liungane kabla ya uchaguzi mkuu wa 2022.Wakiongozwa na Gavana wa Meru Kiraitu Murungi na mwenzake wa Machakos Alfred Mutua, viongozi hao wanasema kwamba kuungana kwa eneo hilo kisiasa kutawapa wakazi nguvu za kutetea maslahi yao katika serikali ya kitaifa kwenye uchaguzi mkuu ujao.

Uliokuwa mkoa wa Mashariki ulihusisha kaunti za Meru, Marsabit, Isiolo, Embu, Machakos, Kitui, Makueni na Tharaka Nithi. Wakizungumza wiki jana katika eneo la Kiagu, Imenti ya Kati katika kaunti ya Meru, magavana hao walisema kwamba vyama vya kisiasa vilivyo na mizizi eneo hilo vinapaswa kuungana ili liwe na nguvu kwenye uchaguzi mkuu ujao.

“Tunahitaji muungano mkubwa ambao utaleta pamoja kaunti nane za mashariki ya Kenya ambao utatusaidia kutoa mgombeaji wa urais katika uchaguzi mkuu ujao,” alisema Gavana Mutua. Wadadisi wa siasa wanasema kuungana kwa kaunti hizo kunaweza kuwa pigo kwa umoja wa jamii za Agikuyu, Ameru na Aembu ambazo zimekuwa zikishirikiana kisiasa chini ya muungano wa GEMA.

“ Itaamanisha kuwa jamii za Ameru na Aembu zitajitenga na GEMA na kuwa pigo kwa umoja wa kaunti za eneo la Mlima Kenya. Hii inawezekana ikizingatiwa kuwa viongozi wa eneo la Mlima Kenya Magharibi wamepinga kutawazwa kwa Spika wa Bunge la Kitaifa Justin Muturi kuwa msemaji wa jamii pana ya GEMA,” asema mdadisi wa siasa Gerald Njau.

Bw Muturi anatoka Embu ambayo ni mojawapo ya kaunti za uliokuwa mkoa wa Mashariki. Mji wa Embu ulikuwa makao makuu ya mkoa huo. Wadadisi wanasema kwamba mgawanyiko kuhusu kutawazwa kwa Muturi na kusambaratika kwa chama cha Jubilee, huenda kukachangia kuundwa kwa muungano huo mpya wa kaunti za eneo pana la Mashariki.

Kwa mujibu wa takwimu za IEBC, kuna zaidi ya wapigakura 4 milioni waliosajiliwa katika kaunti hizo nane. Bw Kiraitu ambaye ametangaza kuwa ataunda chama kipya cha kisiasa alisikitika kwamba kwa muda mrefu, eneo la mashariki ya Mlima Kenya limechukuliwa kama mgeni katika siasa za nchi tangu uhuru.

Gavana huyo wa chama cha Jubilee ametangaza azma ya kuunda chama cha eneo la Mlima Kenya Mashariki atakachotumia kwenye uchaguzi mkuu wa 2022. Kwa upande wake, gavana Mutua ni kiongozi wa chama cha Maendeleo Chap Chap na ametangaza kuwa atagombea urais kwenye uchaguzi mkuu wa 2022.

“Tumechoka kuwa watazamaji na kuchukuliwa kama wageni katika ngoma ya siasa kwa miaka mingi. Wakati huu, eneo la Mshariki ya Mlima limefumbua macho na tuko tayari kuungana na wenzetu kama Mutua, Kalonzo Musyoka (kiongozi wa chama cha Wiper) Charity Ngilu ( Narc) na vyama vingine ambavyo vinatetea maslahi yetu ya kisiasa kwa kuwa sasa tunafufua umoja wetu,” alisema Bw Kiraitu.

  • Tags

You can share this post!

36 kuhojiwa kujaza nafasi 4 za makamishna IEBC

Mahakama: Ni wakati Rais akubali miito