CHAMA Cha ODM kimeamua kuwatuza wanasiasa watakaoshawishi watu kujiunga nacho, badala ya kuelekea kwa UDA.
Viongozi wakuu wa chama hicho waliahidi kutoa zawadi kwa wajumbe ambao wataongoza usajili wa wanachama zaidi.
Zawadi hizo zitatolewa kwa wajumbe kutoka kiwango cha kaunti, wadi na eneobunge, ili kukabiliana na chama tawala cha United Democratic Alliance (UDA) ambacho kimeanza kupata umaarufu.
Kinara wa ODM, Bw Raila Odinga akizindua usajili huo eneo la Mbita, Homa Bay, aliwataka vijana wajiunge kwa wingi na kuwa wanachama.
“Usajili wenu ndio utakaoamua hatua yangu ya kisiasa. Ninaomba kila mtu aliye na kitambuisho kujiandikisha na kuwa mwanachama,” alisema Bw Raila. Mbinu hii itatumika kupunguza makali ya UDA ambayo kwa sasa imepata wanachama wengi.
Gavana Gladys Wanga, aliye mwenyekiti wa chama hicho eneo hilo, alitangaza kutuza wajumbe watakaofikisha asilimia 100 ya usajili huo.
“Tunajulikana kwa kuwa namba moja na tunataka kuongoza katika usajili wa chama pia,” alisema. Kulingana na mwenyekiti wa Kitaifa, John Mbadi, eneobunge la Rangwe ndilo lenye idadi ndogo ya wanachama waliosajiliwa kwa asilimia 47 likifuatiwa na Kasipul lenye asilimia 52.
Haya yanajiri huku UDA ikinuia kuongeza idadi yao zaidi.