• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 7:53 AM
Safaricom ilichangia Sh557 bilioni kwa pato la taifa – Ripoti

Safaricom ilichangia Sh557 bilioni kwa pato la taifa – Ripoti

Na LEONARD ONYANGO

KAMPUNI ya Safaricom ilichangia asilimia 5.2 ya pato la taifa (GDP) katika mwaka wa matumizi ya fedha wa 2020/2021.

Ripoti kuhusu uthabiti wa biashara inaonyesha kuwa kampuni hiyo ya mawasiliano ya simu, ilichangia Sh557.1 bilioni katika uchumi nchi kati ya Aprili 1, 2020 na Machi 31, 2021.

Ripoti hiyo iliyoandaliwa na Safaricom, inaonyesha kuwa kampuni hiyo ilitoa ajira za moja kwa moja kwa watu 190,273 ndani ya kipindi hicho.

Mwenyekiti wa kampuni ya Safaricom, Michael Joseph aliyekuwa akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa ripoti hiyo jijini, alisema zaidi ya Wakenya milioni moja walinufaika na ajira zisizo za moja kwa moja kutokana na huduma zinazotolewa na kampuni hiyo.

Safaricom iliyo na zaidi ya wateja milioni 31, inadhibiti asilimia 64 ya soko la mawasiliano ya simu nchini.Ripoti iliyotolewa na Mamlaka ya Mawasiliano (CA) majuzi inaonyesha kuwa asilimia 68.2 ya Wakenya waliwasiliana kwa kutumia laini ya Safaricom kwa njia ya sauti kati ya Aprili na Juni, 2021.Kati ya Aprili 1, 2020 na Machi 31, 2021, Safaricom ilijipa pato la Sh82 bilioni kutokana na mawasiliano ya sauti

.“Lengo letu kuu ni kuhakikisha kuwa tunabadilisha maisha ya watu,” akasema Bw Joseph.

Wakati huo huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Safaricom, Peter Ndegwa, alisema kwamba kampuni hiyo imepanda jumla ya miti 650,000 katika juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

“Kampuni ya Safaricom inalenga kupanda miti milioni 5 ndani ya miaka mitano ijayo,” akasema Bw Ndegwa.

You can share this post!

Taita Taveta huru kutoza kodi miji inayozozania na Kaunti...

Historia ya Malindi kama mji wa kifahari Uswahilini