NA CHARLES WASONGA
MKURUGENZI wa Idara ya Masuala ya Sheria katika Bunge la Kitaifa Samuel Njoroge sasa ndiye Karani mpya wa bunge hilo.
Hii ni baada ya wabunge Jumanne, Novemba 1, 2022 kupitisha ripoti ya Tume ya Huduma za Bunge (PSC) iliyopendekeza uteuzi wa Bw Njoroge kujaza nafasi hiyo iliyosalia wazi baada ya kustaafu kwa Bw Michael Sialai Aprili 2022. Atahudumu kama Karani wa saba wa bunge hilo tangu uhuru.
Katika kura iliyopigwa wakati wa kikao cha alasiri wabunge 162 waliunga mkono ripoti hiyo ya PSC huku 94 wakipinga.
“Kufuatia matokeo ya kura hiyo ninatangaza kwamba hoja hiyo imepita na sasa Bw Samuel Njoroge ndiye Karani wa Bunge la Kitaifa,” akatangaza Spika Moses Wetang’ula baada ya kukamilika kwa zoezi hilo.
Ripoti hiyo ya PSC iliwasilishwa bungeni na kamishna wa tume hiyo Aden Keynan (Mbunge wa Eldas).