NA JOSEPH NDUNDA
Mwanamume mwenye umri wa miaka 39 ambaye anadaiwa kumpa ujauzito binti wa jirani yake mwenye umri wa miaka 12 ameshitakiwa kwa unajisi.
Bw Erastus Maingi Kavita, seremala katika mtaa wa Soweto, Nairobi, anadaiwa kumnajisi mtoto huyo tarehe tofauti kati ya 2022 na Oktoba 24 mwaka huu.
Anakabiliwa na shtaka mbadala la kufanya kitendo cha aibu na mtoto mdogo kwa kumgusa kimakusudi na isivyostahili.
Kavita nusura auawe na umma baada ya mtoto huyo kufichua kwamba alikuwa akimnajisi na kumpa Sh20 au Sh10.
Mama ya msichana alichukua hatua baada ya binti yake kukiri kwamba mshtakiwa alikuwa akimdhulumu kimapenzi.
Baada ya kuhojiwa, msichana alikiri kwamba Kavita alikuwa akimshawishi kuingia katika nyumba yake na kisha kumnajisi.
Kavita alikanusha mashtaka mbele ya Hakimu Mwandamizi wa Mahakama ya Makadara, Erick Mutunga. Kupitia wakili wake Robi Keboye, aliomba aachiliwe kwa dhamana nafuu akisema alihitaji matibabu.
Aliachiliwa kwa dhamana ya Sh300,000 na mdhamini wa kiasi sawa au pesa taslimu Sh200,000 baada ya kuthibitishia mahakama kwamba hawezi kutoroka.
Kesi hiyo itatajwa Desemba 13 mwaka huu.