NA ALEX KALAMA
AWAMU ya nne ya upasuaji wa miili iliyoondolewa kwenye makaburi yaliyofukuliwa katika msitu wa Shakahola imekamilika hii leo Jumanne huku ikibainika kuwa miili miwili kati ya 26 iliyofanyiwa upasuaji ilikuwa ya wanawake waliofariki wakiwa wajawazito.
Kulingana na ripoti ya upasuaji huo iliyotolewa na mwanapathojia mkuu wa serikali Dkt Johansen Oduor, asilimia kubwa ya miili hiyo haikubainika chanzo cha vifo vya watu hao kutokana na kuharibika kupita kiasi.
Ripoti hiyo aidha imeonyesha kuwa miili 14 ilikuwa ya watu wazima huku 10 ikiwa ya watoto.
Wakati huo huo, daktari huyo wa upasuaji wa miili amebainisha kuwa serikali haijaanza kutoa miili kwa baadhi ya familia kutokana na uchunguzi wa chembechembe za vinasaba – DNA – ambao bado unaendelea.
Vile vile Dkt Oduor amedokeza kuwa wananchi watafahamishwa kuhusu idadi kamili ya familia zilizotambua miili ya wapendwa wao baada ya kupokea ripoti kutoka kwa maabara ya serikali inayofanya uchunguzi wa DNA.