Nina umri wa miaka 32. Mpenzi wangu ana familia. Tumekuwa katika uhusiano kwa muda mrefu sasa anataka nimpe mtoto. Amegharamia matumizi yangu yote na ameahidi atashughulikia malezi ya mtoto. Waonaje?
Wewe bado mchanga na sielewi kwanini umeamua kupendana na mtu aliye na mke, badala utafute mume wako mwenyewe. Hata kama ameahidi kukutunza wewe na mtoto wenu, huna hakika atatimiza ahadi yake. Tafakari hayo.
Nimeolewa na mwanamume aliye mdogo wangu kiumri. Tunapendana sana lakini nimegundua anajipenda zaidi. Ninalazimika kumdekeza ili kudumisha mapenzi nyumbani.
Raha ya mapenzi ni kupendana. Yakizidi, wahusika hudekezana. Sioni ubaya wowote kwako kumdekeza bora tu kitendo hicho kinasaidia kukoleza penzi lenu.
Ninafanya kazi katika kampuni ya mtu binafsi. Mke wa bosi anashuku nina uhusiano na mumewe ilhali hakuna chochote. Ameniuliza mara kadhaa na bado hajaamini. Nifanye nini?
Tabia kama hiyo inatarajiwa kutoka kwa mke wa bosi hasa kama unafanya kazi kwa karibu na mumewe. Lakini hufai kuogopa kama hakuna chochote kinachoendelea kati yenu. Ninaamini atachunguza na atajua ukweli.
Kuna jambo linanitatiza moyoni kuhusu mpenzi wangu. Kuna mwanamke amekuwa akiwasiliana naye na ninashuku anamtaka ama tayari ni wapenzi. Nipe ushauri.
Kama mawasiliano kati yao yanahusu mapenzi, hiyo ni wazi kuwa anakucheza. Lakini kama ni mazungumzo ya kawaida, basi huenda ni marafiki tu. Itakuwa heri ukimuuliza ili ujue ukweli.