• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 2:35 PM
TAHARIRI: Sekta ya elimu yahitaji mageuzi

TAHARIRI: Sekta ya elimu yahitaji mageuzi

NA MHARIRI

SHULE zinafunga wiki hii ili kukamilisha muhula wa kwanza katika kalenda mpya ya elimu nchini. Kalenda ya elimu ilivurugwa kutokana na ujio wa janga la corona ambalo limetatiza shughuli mbalimbali katika ulimwengu kwa jumla.

Ili kufidia muda uliopotea, kalenda ya shule imebadilishwa kwa kupunguzwa pakubwa ili kuerejesha hali ya kawaida. Kutekeleza mabadiliko hayo kumeibuka kuwa changamoto kuu kwa wanafunzi, walimu na wazazi.

Hata hivyo, mabadiliko hayo ni ya muda mfupi tu, makusudio yakiwa kuhakikisha kwamba kalenda ya zamani ya masomo shuleni inachukua mkondo wake.

Hata hivyo, serikali inapaswa kutathmini utaratibu huo. Baada ya mwaka mzima wa utekelezaji wa mpango huo, mambo mengi yameibuka na yanapaswa kuibua mafunzo tele kwa wadau wanaoutekeleza kwa manufaa ya wanafunzi katika siku zijazo.

Changamoto kuu inayokabili wazazi kwa sasa ni suala la karo. Wanapaswa kulipa karo kwa mfuatano mfupi na pia kuwapa nauli ya watoto wao wanaporejea shuleni, zaidi ya kuhakikisha kwamba mahitaji yao yote ya kiakademia yamekidhiwa barabara.

Masaibu haya yote yanatokana na ujio wa tandavu la corona, ambalo limevuruga kila sekta ya kitaifa, ya elimu ikiwa yenye kuvurugwa pakubwa.

Hivyo basi, Wizara ya Elimu inapaswa kuwazia njia mwafaka za kusaka suluhu za matatizo yanayoikabili kwa sasa.

Ikumbukwe kuwa Wizara hii ilipunguza karo mwanzoni mwa muhula na itakuwa busara tupu iwapo karo hiyo itaendelea kupunguzwa hivyo hadi mwisho wa mwaka ili kuwapa wazazi nafasi ya kutafuta pesa.

Shule ambazo zimeongeza karo zinapaswa kumulikwa na kuadhibiwa na serikali kwa kuwapa wazazi zigo zaidi ya lile linalowaelemea sasa hivi.

Serikali pia inapaswa kuhakikisha kwamba likizo fupi za kati ya mihula zinaondolewa kwa muda kwa sababu zina gharama pia kwa mzazi. Si sawa kwa wanafunzi kufunga kwa likizo fupi, ilhali mihula yenyewe imefupishwa.

Utoaji wa basari nao pia unapaswa uende sambamba na kalenda ya shule na wanafunzi zaidi waweze kupokea ufadhili huo, kutokana na ukweli kwamba familia nyingi zimepoteza mapato kutokana na corona.

Muhimu zaidi ni kuwaandaa watahiniwa wa kidato cha nne na darasa la nane kwa mitihani ya kitaifa ambayo inajongea.

You can share this post!

Mzozo wa DPP na DCI waanikwa na kesi ya mauaji ya Cohen

Taita Taveta huru kutoza kodi miji inayozozania na Kaunti...