• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 8:55 AM
Tineja akiri kuua afisa mkuu wa fedha wa Nairobi Hospital, Eric Maigo

Tineja akiri kuua afisa mkuu wa fedha wa Nairobi Hospital, Eric Maigo

Na RICHARD MUNGUTI

MSHUKIWA mkuu katika mauaji ya kinyama aliyekuwa Mkurugenzi wa Uhasibu katika Nairobi Hospital Erick Maigo alisababisha mshangao mkuu katika Mahakama ya Milimani alipokiri alitekeleza uhalifu huo.

Bi Anne Adhiambo Ouma almaarufu Nut alikubali shtaka la kumuua Maigo alipofikishwa mbele ya Jaji Kanyi Kimondo aliposomewa shtaka.

Lakini Jaji Kimondo aliyemwuliza mara mbili kama ameelewa shtaka dhidi yake Adhiambo, hakupitisha hukumu ila aliamuru Adhiambo azuiliwe kwa wiki mbili atathmini upya maungamo yake.

“Je umeelewa shtaka linalokukabili adhabu yake ni kunyongwa au kufungwa jela maisha ukipatikana na hatia,”Jaji Kimondo alimweleza Adhiambo.

Lakini Adhiambo alijibu na kusema, “Mheshimiwa nimeelewa shtaka linalo nikabili. Ni kweli nilimuua Eric Maigo.” Jibu hilo lilimduwaza wakili Samuel Ayora anayemtetea.

Bw Ayora aliomba kesi hiyo iahirishwe kwa wiki mbili kumpa muda ashauriane na mshtakiwa.

Hata hivyo upande wa mashtaka ulisema Adhiambo yuko na akili timamu na anaelewa achosema. Pia Jaji Kimondo alifahamishwa mshtakiwa yuko na umri unaozidi miaka 18 na “anaelewa anachojibu.”

Bw Ayora alieleza Taifa Leo katika mahojiano maalum alikuwa amemshauri Adhiambo akanushe shtaka.

“Nilikuwa nimemshauri Adhiambo akane shtaka lakini sijui sababu ya kubadilisha nia na kukiri aliua,” Bw Ayora aliambia Taifa Leo.
Wakili huyo aliomba mshtakiwa azuiliwe katika kituo cha polisi akidai umri wake uko chini ya miaka 18.

Lakini Jaji Kimondo alimkatiza Bw Ayora akisema,“ Tayari Hospitali Kuu ya Kenyatta ilimpima mshtakiwa umri na kutoa ripoti kwamba ni mtu mzima.”

Mahakama ilimweleza Bw Ayora anahitaji muda kushauriana na mteja wake kabla ya kusomewa upya shtaka Novemba 8,2023.

  • Tags

You can share this post!

Naftali Kinuthia apatikana na hatia ya kumuua mwanachuo Ivy...

Marioo asema ameshapata Sh6 milioni za kumuoa Paula Kajala

T L