NA WINNIE ONYANDO
MWANAHARAKATI Francis Awino ametangazwa kama kiongozi mpya wa vuguvugu la Bunge la Mwananchi.
Tangazo hilo lilitolewa na mwenyekiti wa kamati ya uchaguzi wa vuguvugu hilo Robert Kiberenge, katika bustani ya Jeevanjee jijini Nairobi mnamo Alhamisi.
“Kutokana na mamlaka niliyopewa kama mwenyekiti wa Bunge la Mwananchi, namtangaza Fancis Awino kuwa ndiye mshindi wa kiti cha urais wa vuguvugu letu. Naibu wake ni Maurice Masinga,” Bw Kiberenge alitangaza.
Bw Awino sasa amechukua nafasi ya Calvince Okoth almaarufu Gaucho ambaye amekuwa mojawapo wa viongozi walioongoza umaarufu wa vuguvugu hilo nchini.
Japo uchaguzi ulipangwa kufanyika Agosti mwaka huu kama ilivyoainishwa kwenye katiba ya vuguvugu hilo, Bw Kiberenge alisema walilazimika kuahirisha uchaguzi huo kutokana na maandamano yaliyokuwa yakiendelea nchini.
Katika uchaguzi wa Alhamisi (Desemba 7,2023) polisi waliwavuruga wapiga kura na kuulazimisha kamati ya uchaguzi kusimamisha mchakato huo.
Hii ilimlazimisha Bw Kiberenge kuhesabu kura ambazo zilipigwa kabla ya polisi kuvuruga uchaguzi wao.
Kati ya kura zote zilizopigwa, Bw Awino alipata kura 37.
“Hii ni kwa sababu si wote waliosajiliwa kupiga kura walifanya hivyo,” akaeleza Bw Kiberenge.