• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 8:50 AM
Arsenal wataruka kamba ya Aston Villa ugani Villa Park?

Arsenal wataruka kamba ya Aston Villa ugani Villa Park?

LONDON, Uingereza

Tottenham ya kocha Ange Postecoglou walitangulia kufunga kupitia kwa Cristian Romero dakika ya 11, lakini wakaishia kunyamazishwa na West Ham kupitia mabao ya kipindi cha pili kutoka kwa Jarrod Bowen na James Ward-Prowse.

Ni mechi ya tano mfululizo Tottenham wamekosa ushindi. Wana alama moja kutoka michuano hiyo na kusababisha Postecoglou akasolewe vikali na mashabiki. Nahodha Son Heung-min alitaja wachezaji wenzake kama “vifyefye” naye Romero akaomba msamaha kwa msururu wa matokeo duni kutoka kambini mwao.

Newcastle walilimwa 3-0 na Everton wanaoendelea kufufuka tangu wapokonywe alama 10 kwa kuvunja sheria za matumizi ya kifedha majuzi. Dwight McNeil, Abdoulaye Doucoure na Beto walifungia Everton katika dakika za lala-salama.

Jumamosi Arsenal itaanza mchuano dhidi ya kocha wake wa zamani Unai Emery anayenoa Villa ikiwa na rekodi nzuri ya ana kwa ana. Vijana wa kocha Mikel Arteta wamepepeta Villa mara nne mfululizo kwa jumla ya magoli 10-5.

Hata hivyo, wanabunduki hao wanaojivunia wachezaji matata wakiwemo Bukayo Saka, Declan Rice na Gabriel Martinelli, wanafaa kufahamu fika kuwa Villa hawajapoteza mechi 14 mfululizo ligini nyumbani Villa Park.

Wapinzani wa mwisho kuzuru uga huo ni mabingwa watetezi Manchester City ambao walilishwa kichapo cha bao 1-0. Ollie Watkins ni mmoja wa wachezaji hodari kambini mwa Villa wanaoweza kusambaratisha kampeni ya Arsenal.

Vijana wa Arteta watadumisha uongozi wa alama mbili juu ya jedwali wakipata ushindi nao nambari mbili Liverpool wachape Crystal Palace (14) katika mechi itakayofungua siku. Ugani Selhurt Park, macho yatakuwa kwa wavamizi Odsonne Edouard (Palace) na Mohamed Salah (Liverpool) katika mechi hiyo imeshuhudia sare mara mbili mfululizo.

Manchester United ya kocha Erik ten Hag huenda ikang’oa Tottenham katika mduara wa tano-bora ikipata ushindi dhidi ya nambari 15 Bournemouth inavyotarajiwa.

Ratiba ya EPL (Uingereza):

Desemba 9 – Crystal Palace v Liverpool (3.30pm), Wolves v Nottingham Forest (6.00pm), Brighton v Burnley (6.00pm), Sheffield United v Brentford (6.00pm), Manchester United v Bournemouth (6.00pm), Aston Villa v Arsenal (8.30pm); Desemba 10 – Luton Town v Manchester City (5.00pm), Fulham v West Ham (5.00pm), Everton v Chelsea (5.00pm), Tottenham Hotspur v Newcastle (7.30pm).

  • Tags

You can share this post!

Wasiwasi waibuka Embu watu 15 wakijitoa uhai ndani ya miezi...

Vuguvugu la Bunge la Mwananchi lachagua rais mpya

T L