NA RICHARD MAOSI
LICHA ya sehemu nyingi katika barabara kuu ya Nairobi kuelekea Mau Summit kutajwa kuwa hatari, bado wafanyibiashara wanahatarisha maisha kwa kutafuta wateja hadi katikati mwa barabara.
Wengi wao hutimka kwa kasi kuyakimbilia malori ya masafa marefu au matatu bila kutilia maanani usalama wa kibinafsi
Unapofika Kinungi, Fly Over na Limuru utashuhudia ukungu mzito nyakati za asubuhi na hali huwa mbaya pale mvua inapoanza kunyesha.
“Isitoshe ajali huongezeka wakati wa shamrashamra za sherehe za mwisho wa mwaka kama vile Krismasi ikizingatiwa kuwa shughuli za uchukuzi huwa zimepamba moto wakazi wengi wakijaribu kuwahi kufika vijijini” asema James Kibe mkaazi Flyover.
Analaumu Mamlaka ya Kitaifa ya Uchukuzi na Usalama (NTSA) kwa kushindwa kudhibiti visa vya ajali katika barabara ya Nairobi -Nakuru, licha ya kufahamu kuwa ni eneo lenye shughuli nyingi za uchukuzi.
Zaidi ya mara moja, Kibe anasema ameshuhudia NTSA wakifukuzana na matatu ambazo huwa zimekiuza sheria za barabarani bila kujali kuwa ni eneo ambalo huwa na idadi kubwa ya wafanyibiashara kandokando au katikati mwa barabara.
Licha ya kufahamu kuwa ni mojawapo ya maeneo hatari zaidi nchini, anapendekeza wafanyibiashara kutengewa sehemu maalum ya kuuzia na matuta kuongezwa barabarani.
Ni takriban kilomita 36 kutoka kituo cha kibiashara cha Kikopey hadi jijini Nakuru na humchukua dereva dakika 25 hivi kufika.
Januari 2023 watu saba walipoteza maisha yao katika ajali mbaya iliyofanyika kwenye kituo cha Kibiashara cha Kikopey.
Hii ni mojawapo ya barabara yenye kumbukumbu nyingi kutokana na idadi kubwa ya ajali zinazoshuhudiwa na kuwaacha wengi kuwa mayatima au wajane.
Hapa utakumbana na glasi zilizopasuka na mabaki ya magari ambayo awali yamehusika kwenye ajali ya barabarani jambo linalowafanya wakazi kubatiza eneo hili jina “Highway to Hell.”
Highway to Hell, kwa Kiswahili inamaanisha barabara ya kuelekea jehanamu.
Njia hii hufululiza kutoka eneo la Sachangwan, Migaa, Mau Summit mpaka jijini Naivasha.
Isitoshe ripoti ya usafiri barabarani inaonyesha kuwa visa vya ajali barabarani vimewaangamiza watu wengi humu nchini, ikilinganishwa na maradhi ya Ukimwi au Malaria.