NA ALEX KALAMA
NI afueni kwa wahudumu wa afya ya jamii wa kujitolea (CHVs) katika Kaunti ya Kilifi baada ya bunge la kaunti hiyo kupitisha mswada wa kuwalipa marupurupu.
Akizungumza katika wadi ya Dabaso, eneobunge la Kilifi Kaskazini, Waziri wa Afya wa Kilifi Peter Mwarogo alisema kuwa sasa ni rasmi kuanzia mwezi huu wa Julai, wahudumu hao wa kujitolea wataanza kupokea marupurupu yao, pamoja na kusajiliwa katika mpango wa Bima ya Kitaifa ya Afya ya NHIF
“Kuanzia kesho wahudumu hao watakuwa wakilipwa na serikali ya kaunti. Pia wafahamu kwamba tumeshawasajili kwa bima ya afya ya NHIF na wiki moja ama mbili hivi tutawaita waje kwa mkutano na watapokea,” alisema Bw Mwarogo.
Afisa huyo alisema kilio cha wahudumu hao kiliwafikia.
“Kilio cha wahudumu kilitufikia na tulijadiliana na mswada ukapelekwa katika bunge la kaunti ambalo liliupitisha na hivi sasa watakuwa wakipokea marupurupu yao kila mwezi kuanzia mwezi huu wa Julai,” aliongeza Bw Mwarogo.
Mmoja wa wanufaika, Sumira Faraji, ambaye anahudumu katika wadi ya Dabaso, alionyesha furaha yake kutokana na hatua hiyo na kudokeza kuwa malipo hayo yatawapa motisha zaidi wa kutekeleza wajibu wao.
“Inapata kama miaka 20 tokea nianze kazi hii. Tunashukuru kilio chetu kimeangaziwa na japo hatujajua tutalipwa pesa ngapi, tunafurahi kusikia ya kuwa tutalipwa hayo marupurupu. Hii inatupa motisha sisi wahudumu wa afya wa nyanjani,” alisema Bw Faraji.
Naye Tomick Yeri, pia kutoka Dabaso, ameipongeza serikali ya kaunti kwa kuwasajili wahudumu hao katika bima ya afya ya NHIF na kuelezea kuwa hatua hiyo itatatua matatizo yao ya kiafya.
“Kuwekwa kwa NHIF kunatusaidia sana kwa sababu sasa nikiugua nitapata matubabu bila kuhangaika,” alisema Bw Yeri.