NA WINNIE ONYANDO
MADIWANI wa mrengo wa United Democratic Alliance (UDA) katika Kaunti ya Nairobi, sasa wanakusanya saini ili kuwang’oa mamlakani viongozi wao katika bunge la kaunti hiyo.
Kwa sasa, Anthony Kiragu ndiye Kiongozi wa Wachache katika bunge hilo huku diwani wa wadi wa Nairobi Kusini Bi Waithera Chege akiwa naibu wake.
Naye Mark Mugambi Macharia ndiye Kiranja wa Wachache katika bunge hilo.
Lakini sasa madiwani hao wakiongozwa na Bi Waithera, wanasema hawana imani tena na Bw Kiragu na Bw Mugambi.
Jumla ya madiwani 35 wa muungano wa UDA wametia saini ombi la kuwaondoa viongozi hao wawili kwa msingi kuwa wameshindwa kuwaleta pamoja madiwani wa UDA.
Kikao hicho kilichoongozwa na Jeremiah Themendu, kilisema kwamba viongozi hao wamekosa uadilifu wanapotekeleza wajibu wao.
Kadhalika, madiwani hao pia walisema kuwa viongozi hao wameshindwa kuwawakilisha vyema bungeni na kwamba wawili hao ni wabadhirifu.
“Kumekuwa na pendekezo la kuwang’oa madarakani viongozi hao wawili,” inasema sehemu ya kumbukumbu za mkutano huo.
Hata hivyo, Bw Kiragu alisema kwamba anafahamu kuwa kuna njama ya kuwang’oa uongozini.
“Nina ufahamu kuwa madiwani wanakusanya saini ili kutuondoa mamlakani. Ni hatua ya watu wenye wivu,” akasema Bw Kiragu.