NA SAMMY KIMATU
WAKAZI katika mitaa ya mabanda ya Mukuru, kwenye tarafa ya Landi Mawe, South ‘B’, wameonywa vikali dhidi ya kuchafua mazingira.
Chifu wa eneo hilo, Bw Peter Maroa alionya wanaogeuza Mto Ngong na daraja la Kayaba/Hazina kuwa dampo.
Bw Maroa alizungumza hayo mnamo Jumamosi alipoongoza hafla ya kusafisha mtaa wa mabanda wa Mukuru-Kayaba.
“Leo, maafisa wa utawala kutoka tarafa ya Landi Mawe tukishirikiana na kikundi cha HAND IN HAND pamoja na serikali ya kaunti ya Nairobi tumeungana kusafisha mtaa na kuwa kielelezo na kioo cha jamii ili watuige katika kampeni ya kusafisha mazingira kwa nia ya kuwa na mazingira safi, bora na yaliyo salama kwa watu kuishi,” Bw Maroa akasema.
Aliongeza kwamba walizibua mitaro ya kupitisha majitaka, wakafagia barabara huku malori ya kaunti ya Nairobi yakizoa taka kupeleka kwenye dampo la Dandora.