Na SAMMY WAWERU
UTATA umeibuka kuhusu umiliki wa shamba la ekari 800 Kilifi linalosemekana kuwa la pasta tata Paul MacKenzie.
Inspekta Jenerali Mkuu wa Polisi, IG Japhet Koome alisema Jumatatu kwamba tayari baadhi ya watu wamejitokeza wakidai umiliki wa ardhi hiyo.
“Ardhi hii ina mzozo. Baadhi wamejitokeza wakidai wanaimiliki,” IG Koome akaambia wanahabari alipozuru Shakahola, Malindi ambako shughuli ya ufukuzi makaburi inaendelea.
Mhubiri MacKenzie anatuhumiwa kuhadaa wafuasi wa Kanisa lake la Good News International, akiwashikiza kufunga bila kula wala kunywa ahadi ikiwa wakifa watakutana na Yesu.
Bw Koome alisema tangu kuanza kwa oparesheni ya ufukuzi wa makaburi yenye miili ya waumini wa MacKenzie, miili 39 imetolewa.
Idadi jumla ya waliothibitishwa kufariki kutokana na hadaa za MacKenzie, imefika 47.
Hali kadhalika, watu 27 wameokolewa wakiwa wamedhoofika kiafya.
Oparesheni hiyo inaendeshwa na Idara ya Upelelezi wa Jinai na Uhalifu (DCI).
Mchungaji huyo anazuiliwa na polisi uchunguzi ukiendelea, kabla kufunguliwa mashtaka.