NA STANLEY NGOTHO
BARAZA la Kitaifa la Mitihani Nchini (KNEC) limewahakikishia watahiniwa wa Mtihani wa Kitaifa wa Darasa la Nane (KCPE) na ule wa Gredi ya Sita (KPSEA) kwamba mitihani hiyo imelindwa na hakutatokea udanganyifu wowote.
Akiongea Ijumaa katika Shule ya Msingi ya Athi River wakati watahiniwa walipokuwa wakifanyiwa majaribio, Afisa Mkuu Mtendaji wa baraza hilo Dkt David Njeng’ere alisema kuwa mitihani hiyo itaendelea bila shida yoyote.
Aliwataka watahiniwa wa KCPE na KPSEA kujiandaa vizuri, akisema mitihani hiyo itasimamiwa vizuri chini ya ulinzi mkali.
“Mtihani wa KPSEA utafanywa katika vituo 32,000 na ule wa KCPE utafanywa katika vituo 28,000 kote nchini. Mikakati mikali imewekwa kulinda mitihani hiyo ili isivuje hata kidogo,” Dkt Njeng’ere akasisitiza.
Mitihani hiyo pia itafanyika katika vituo vingine 576 visivyo katika mazingira ya shule.
Dkt Njeng’ere alionya wazazi dhidi ya kutapeliwa na walaghai wanaodai wanaweza kuwauzia karatasi za mitihani, akisema watapoteza pesa zao.
“Hakuna mtu ambaye ameweza kuingilia mitihani hiyo iliyohifadhiwa katika makontena. Kwa hivyo, wazazi wasidanganywe na walaghai eti wanauziwa karatasi za mitihani ya KCPE au KPSEA,” akaongeza.
Mitihani hiyo inaaza Jumatano hadi Ijumaa juma lijalo.
TAFSIRI NA: CHARLES WASONGA